Jumanne, 27 Septemba 2016

TAARIFA YA WIZARA YA AFYA KWA UMMA (HALI YA UPATIKANAJI WA DAWA NCHINI)

indexHivi karibuni kumekuwepo na taarifa iliyotolewa na Taasisi isiyo ya kiserikali inayofuatilia masuala ya Afya ,Sikika pamoja na baadhi ya vyombo vya habari kuwa MSD inakabiliwa na upungufu wa dawa na kutoa takwimu kuwa kuna makopo 173 tu ya dawa aina ya Paracetamol nchini.
Wizara inapenda kutoa ufafanuzi kuhusu taarifa hizi kama ifuatavyo.
Kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016, MSD ilianza utaratibu wa kununua dawa na vifaa tiba moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji kama jitihada za kuhakikisha kuna upatikanaji endelevu wa mahitaji hayo kwa wananchi.
Wizara kupitia MSD tayari imepokea makopo 10,000 ya vidonge vya Paracetamol ambayo yamekwishasambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.Aidha  mkataba kati ya MSD na mtengenezaji wa ndani wenye   makopo mengine   138,000 ya vidonge vya Paracetamol yenye ujazo wa vidonge 1,000 umekamilika, ambapo  dawa hizo zinategemewa kuanza  kupokelewa kuanzia wiki ya kwanza ya mwezi wa Oktoba 2016.
Aidha, dawa nyingine zilizokuwa zinahitajika zaidi ambazo ni antibiotics na dawa za kupunguza maumivu (Ciprofloxacin, Ceftriaxone, , Diclofenac, Co-trimoxazole, Amoxycyline, Doxycycline na Metronidazole) ziliwasili makao makuu ya MSD na tayari zimekwisha pelekwa   kwenye kanda zote za MSD tayari kwa kusambazwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.
Kwa sasa hali halisi ya upatikanaji wa Dawa MSD ni sawa na 53% kwani kati ya dawa muhimu 135 zinazohitajika ghalani kuna aina 71 ya dawa hizo na nyinginezo ziko kwenye vituo vya kutole huduma. Hali ya upatikanaji wa dawa itaimarika zaidi mwezi Oktoba mwaka huu hasa kutokana na Bohari ya Dawa kutumia mikataba ya muda mrefu na washitiri (Framework contracts) ili kuimarisha upatikanaji wa dawa wa haraka, pindi zinapohitajika kulingana na fedha zinazopatikana.
Vilevile tunapenda kutoa taarifa kwa umma kuwa dawa za Miradi Msonge, ambazo zinatibu na kuzuia magonjwa ya Malaria, UKIMWI, Kifua Kikuu, Ukoma, kichaa cha mbwa, uzazi wa mpango na chanjo mbalimbali zipo za kutosha kwenye Bohari zetu.
Kadhalika, Wizara inapenda kutoa taarifa kuwa hali ya upatikanaji wa chanjo nchini utaimarika zaidi kuanzia tarehe 2 Oktoba, 2016 baada ya kupokea shehena mpya. Hata hivyo, Wizara inawaomba Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuangalia mwenendo wa shehana zao na kutoa mgawo mpya kwenye maeneo yenye upungufu (stock redistribution)pale kadhia hii inapotokea.
Dkt. Mpoki Ulisubisya
KATIBU MKUU-AFYA
27 Septemba, 2016

0 maoni:

Chapisha Maoni