Alhamisi, 15 Septemba 2016

Serikali itahakikisha waliotekwa nyara Kongo wanapatikana wakiwa salama

719a9907

Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga.
……………………………………………………………………
Na. Immaculate Makilika- MAELEZO
Serikali  imesema kuwa inashirikiana na Serikali  ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuhakikisha kuwa  madereva   wanaoendesha  magari aina ya malori    ambao wametekwa  nyara  jana na waasi wa kikundi  cha Maimai   katika eneo la Namoyo  jimbo la  Kivu kusini  katika nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya  Kongo wanapatikana wakiwa salama.
Hayo yamesemwa  na Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bi. Mindi Kasiga  leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuwakoa watanzania waliotekwa nyara.
“Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Kongo inaendelea kufanya kila jitihada kuhakikisha  madereva hao wanaachiwa huru haraka iwezekanavyo na kurudishwa nchini wakiwa salama”
“ Waasi hao wa Maimai wametoa masaa 24 hadi kufikia  leo wawe wamelipwa kiasi cha Dola 4,000 kwa kila dereva  ili waweze kuwaachia huru  na kutishia  kuwadhuru endapo hawatapata fedha hizo, hivyo basi Serikali imeendelea kuwa na mazungumzo na Serikali ya Kongo ili kupata ufumbuzi wa suala hili” alisema Kasiga
Aliongeza kuwa malori yaliyotekwa nyara ni 12 kati ya hayo nane  ni mali ya mfanyabiashara wa kitanzania  Bw. Azim  Dewji na mengine ni mali za wafanyabiashara kutoka nchini Kenya.
Aidha, Serikali imewataka watanzania  kufahamu  hali ya usalama wa nchi wanazokwenda ili kujikinga na matatizo mbalimbali yanayoweza kuwapata wakiwa katika nchi hizo.

0 maoni:

Chapisha Maoni