Jumamosi, 17 Septemba 2016

UHIKI yatoa mafunzo kwa vijana waliohitimu mafunzo ya ufundi

lim1
Afisa Msimamizi wa Miradi ya Kuweka na Kukopa kutoka Shirika la Uhamasishaji Hifadhi Kisarawe (UHIKI) , Vuai Shame akiongea na waandishi wahabari (hawapopichani) juu ya umuhimu wa vijana waliohitimu mafunzo ya ufundi chini ya mradi wa Uwezeshaji Vijan aKiuchumi (YEE) kupata elimu ya utunzaji wa fedha pamoja na upatikanaji wa mikopo kwa ajili waweze kuimarisha biashara zao.
lim2
Vijana waliohitimu mafunzo ya ufundi chini ya mradi wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi (YEE) wakiwa na vyeti vya utambulisho wa kikundi chao kilichosajiliwa kwajina la YEE Tailoring and Decoration Group na Halmashauri ya Manispaa ya Kisarawe,nyuma kulia ni Mratibu wa Mradiwa YEE Kanda yaMashariki, Adolf Jeremiah.
……………………………………………………………….
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO, Kisarawe.
Shirika la Uhamasishaji Hifadhi Kisarawe (UHIKI) limetoa mafunzo ya kuweka na kukopa fedha kwa vijana waliohitimu mafunzo ya ufundi chini ya mradi wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi (YEE) ili kuwaelimisha jinsi ya kutunza fedha zao.
Mafunzo hayo yametolewa leo katika Kijiji cha Kauzeni, Kata ya Kibuta wilayani Kisarawe ambapo vijana wamefundishwa jinsi ya kupanga, kuchagua na kusimamia shughuli yoyote inayofanywa kwa ajili ya kujiingiza kipato pamoja na umuhimu wa kujiwekea akiba.
Afisa Msimamizi wa Miradi ya Kuweka na Kukopa – Kisarawe, Vuai Shame amesema kuwa kuna umuhimu wa vijana kupata elimu juu ya utunzaji wa fedha pamoja na upatikanaji wa mikopo ili waweze kuimarisha biashara zao na kuona faida inayopatikana kutokana na biashara hizo.
“Kazi ya UHIKI ni kuwasimamia vijana ili waweze kuunda vikundi vya kuweka na kukopa fedha zitakazowasaidia kuendeleza biashara zao, mpaka sasa tumefanikiwa kuwa na vikundi 27 vya vijana vilivyopo katika kata 4 za wilaya yetu lakini bado tunaendelea kuwahamasisha vijana wengine kufanya hivyo kwani vikundi vina faida”, alisema Shame.
Afisa huyo ameongeza kuwa kwa sasa wameamua kuwasajili vijana katika  makundi kulingana na fani walizosomea ili kuwarahisishia kupata mikopo au misaada kutoka sehemu mbalimbali pamoja na kupanua uwanja wa fursa za  kupata tenda kwa wingi.
Aidha, Shame ameishukuru Serikali kwa kuwa bega kwa bega na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali katika kuhakikisha wanawasaidia vijana kujikwamua kutoka kwenye lindi la umasikini kwa kuwapa mikopo vijana walio katika vikundi hivyo ili waimarishe biashara zao na kujiongezea vipato.
Naye Mwenyekiti wa Kikundi cha hisa cha Jitegemee, Yassin Omary amesema kuwa walianzisha kikundi hicho mnamo Februari 2 mwaka huu baada ya kuhitimu elimu ya ufundi chini ya mradi wa YEE ambapo hadi sasa wamefanikiwa kuwekeza jumla ya hisa 1,621,000 zinazowawezesha kujikopesha wenyewe kwa wenyewe kwa ajili ya kutatua changamoto zao.
“Kujiunga kwenye vikundi vya namna hii kuna umuhimu hasa kwa sisi vijana ambao biashara zetu bado changa kwani vinatupa uwezo wa kukopa fedha pale biashara inapoyumba au pale unapotaka kuongeza mtaji kwa ajili ya kuinua biashara yako”,alisema Omary.
UHIKI ni shirika lisilokuwa la kiserikali lililoanzishwa mwaka 2009, ni moja kati ya mashirika yanayowasaidia vijana waliopo chini ya mradi wa YEE unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na kuratibiwa na shirika la Plan International katika kuunda vikundi vya kuweka na kukopa fedha. 

0 maoni:

Chapisha Maoni