Jumapili, 25 Septemba 2016

NEC yaziomba halmashauri kuunga mkono elimu ya mpiga kura

Posted by Esta Malibiche on Sept25.2016 in NEWS

nim1
Hussein Makame-NEC
Tume ya Taifa ya Uchaguzi imewaomba wakerugenzi na wenyeviti wa halmashauri nchini kuwapa ridhaa watendaji na makamishna wa Tume hiyo watakaofika katika maeneo yao ili kutoa elimu ya mpigakura kwenye maeneo yao. Ombi hilo limetolewa na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Bw. Kailima Ramadhani wakati akiwasilisha mada kwenye Mkutano Mkuu wa 32 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) uliomalizika mwishoni mwa wiki hii mjini Musoma mkoani Mara. Bw. Kailima aliomba iwapo maafisa uchaguzi au mtendaji na makamishna wa tume watafika maeneo yao wawape fursa ya kukutana na mabaraza ya madiwani na mikutano ya vijiji na mitaa na kukutana na watendaji wengine ili kutoa elimu ya mpiga kura. “Kwa hiyo niwaombe waheshimiwa wenyeviti na wakurugenzi, wale watendaji maafisa uchaguzi kwenye halmashauri zenu au mtendaj na makamishna wa tume wanapofika pale muwape fursa ya kukutana na mabaraza ya madiwani”, alisema Bw. Kailima na kuongeza kuwa: “Niwaombe muwape fursa ya kwenda kwenye mkutano Mkuu wa kijiji au mkutano mkuu wa mtaa, kuwapa fursa ya kukutana na watendaji wengine kwenye eneo lako au kwenye shule za sekondari.Tunaomba muwape ridhaa ya kwenda kutoa elimu hiyo na tunaomba Mungu atuongoze ikifika mwaka 2019 asiwepo mtendaj ambaye hajui tume angalau majukumu yake.” Alisema lengo la kuwepo kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwenye mkutano huo ni kutoa elimu ya mpiga kura na ambalo nii jukumu la Kikatiba la Tume ya Taifa ya Uchaguzi. “Ukisoma ibara ya 74 ya Katiba ya Jamhuru ya Muungano wa Tanzania ibara ndogo (6) (e) inasema Tume itatekeleza majukumu mengine yote kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge” alifafanua Bw. Kailima na kusisitiza kuwa: “Ukisoma pia kifungu cha 4 C cha Sheria ya Uchaguzi, Tume inaelekezwa Kutoa elimu ya mpiga kura nchini nzima na kusimamia na Kuratibu Asasi na Taasisi zinazotoa elimu hiyo.” Mkurugenzi huyo wa Uchaguzi alibainisha kuwa uzoefu unaonesha kuwa elimu ya mpiga kura imekuwa ikitolewa wakati wa kipindi cha Uchaguzi Mkuu tu na hata hivyo maeneo mengi yanashindwa kufikika. Alisema madiwani ambao walihudhuria mkutano huo wa ALAT ni wenyeviti wa kamati za maendeleo ya Kata hivyo iwapo diwani akishiba elimu ya mpiga kura atahamasisha elimu hiyo kwa wenyeviti wa vijiji na hatimaye kuhamasisha elimu hiyo ifike hadi kwa wanavijiji. NEC imeweka mikakati mbalimbali ya kutoa elimu ya mpiga kura ambapo katika mkutano huo mbali na kutoa elimu kwa wajumbe wa mkutano huo lakini pia ilitoa elimu hiyo kwenye shule ya Sekondari ya Songe ya mjini Musoma na kukutana na wananchi kuwapa elimu hiyo kwenye maonesho ya mkutano huo.

0 maoni:

Chapisha Maoni