Alhamisi, 29 Septemba 2016

Wanafunzi shule ya msingi Kashai wanaendelea na masomo

Posted by Esta Malibiche on Sept29.2016 in NEWS

shu
Na mwandishi wetu
Tatizo lolote linapotokea katika jamii huambatana na mambo mbalimbali ikiwemo kutembelewa na wageni wakiwemo waandishi wa habari.
Hali hiyo imetokea katika Manispaa ya Bukoba kufuatia tetemeko la ardhi lililoathiri mkoa huo pamoja na miundombinu mbalimbali ambapo shule ya msingi Kashai nayo ilipata athari za tetemeko hilo.
Athari hiyo ya tetemeko ilipelekea chombo kimoja cha habari cha televisheni nchini kuripoti katika taarifa ya habari kuwa shule hiyo imefungwa na wanafunzi wamerudishwa nyumbani mara baada ya kumaliza likizo fupi badala ya kuendelea na masomo.
Taarifa ya kufungwa kwa shule hiyo inakanushwa na aliyekuwa Mwalim Mkuu wa Shule ya Msingi Kashai, Gideon Kenjori Akizungumzia kuhusu suala hilo na kusema kuwa shule haijafungwa na wanafunzi wanaendelea kusoma kama kawaida.
Mwalimu huyo amesema kuwa habari hiyo iliyotangazwa haikuwa na ukweli wowote kwa kuwa wanafunzi wanaendelea na masomo kwa madarasa yote huku akimshangaa mwandishi wa habari aliyetoa habari hiyo na kusema alijitengenezea habari aliyeitaka yeye na sio hali halisi ya shule ya Kashai.
“Shule haijafungwa, mimi sikuja na mwandishi wala sikuwepo,mwandishi alikurupuka na kuenda nyuma na wala hakuja ofisini na hajaonana na sisi, yeye aliripoti ya kwake aliyeyaona na hakuna mtu ambaye aliongea nae, aliandika ya kwake na amepata taarifa alizotaka alikojua” alisema Mwalimu Gideon.
Mwalimu huyo amesema kuwa athari za tetemeko limeharibu vyumba saba vya madarasa ambavyo havifai kutumika, vyumba nane vinaweza kutumika na nyumba ya mwalimu imepata nyufa hatarishi.
Ili kuhakikisha wanafunzi wote wanasoma umefanyika utaratibu wa wanafunzi kusoma kwa awamu ambao ni wanafunzi wa darasa la kwanza na pili na wanafunzi wengine wa darasa la tano na la sita wamehamishiwa katika shule ya msingi Tumaini ambapo kuna madarasa manne yaliyowazi wakati wanafunzi wa madarasa mengine yaliyobaki wanaendelea na masomo shuleni hapo.
Mwl. Gideon ameongeza kuwa uwezo wa kufunga shule haupo chini ya Mwalimu Mkuu bali mamlaka ya kufunga shule inatoka kwa uongozi wa juu ambao ndio wenye uwezo huo, kwa maana hiyo shule haikufungwa.
Katika kuhakikisha wanafunzi wanaendelea na masomo kulingana na ratiba ya muhula wa masomo, Uongozi wa Manispaa ya Bukoba umeagiza walimu ambao nyumba zao hazifai kutumika watafute nyumba za kupanga na manispaa italipia gharama za nyumba hizo wakati utaratibua kukarabati au kujenga nyumba zao unaendelea ili maisha yao yaendelee kama kawaida waweze kutimiza majukumu yao ya kufundisha.

0 maoni:

Chapisha Maoni