Alhamisi, 22 Septemba 2016

MALI ZILIZOPATIKANA KWA NJIA YA RUSHWA NA UFISADI KUTAIFISHWA

mun
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angellah J. Kairuki (Mb) akiongea na vyombo vya habari kuhusu masuala ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania hivi karibuni. (Picha ya Maktaba).
……………………………………………………………………………………………
Makala iliyopita Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  Mhe. Angellah J. Kairuki (Mb) aliongea kuhusu matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Serikalini, pamoja, Matumizi ya Nyaraka za Serikali na Maadili kwa viongozi kwa viongozi wa Umma. Waziri Kairuki aliongea hayo katika Runinga ya Taifa (TBC), makala ya leo ni sehemu ya mwisho na inaangalia mapambano dhidi ya rushwa na mpango wa kunusuru kaya masikini hapa nchini.
Mapambano dhidi ya rushwa
Waziri Kairuki alieleza Serikali imekuwa ikichukua hatua katika kuzuia na kupambana na rushwa nchini mfano kwa kufuatilia fedha za Miradi ya Maendeleo kupitia Ofisi za Kanda za TAKUKURU kwa lengo la kuhakikisha thamani ya miradi inayotekelezwa inaendana na kiasi cha fedha kilichotolewa ambapo ufuatiliaji huo umeiwezesha Serikali kuokoa kiasi cha Shilingi Bilioni 39.34.
“Tumewasilisha majalada 297 kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kwa ajili ya kuombewa kibali cha mashitaka ambapo majalada 229 yalipata kibali cha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani” Waziri Kairuki alifafanua.
Aliongeza mikakati ya serikali ni pamoja na kuhuisha Sheria ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa Na. 11 ya 2007 ili kujumuisha makosa ya uhujumu uchumi na kutaifisha mali zilizopatika na kwa njia ya Rushwa na Ufisadi.
Kuhusu kaya masikini hali ikoje?
Waziri Kairuki alisema Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini ambao utachukua miaka kumi unatekelezwa katika Halmashauri zote za Tanzania Bara pamoja na Zanzibar.
“Katika kipindi cha miaka minne mpango umetekelezwa Vijiji, Mitaa na Shehia 9,960 ambayo ni sawa na wastani wa asilimia 70. Kaya 1,358,268 zimetambuliwa ambapo kati ya hizo, Kaya 1,110,377 zimeandikishwa” Waziri Kairuki alisena na kuongeza kaya 1,110,377 zimehawilishiwa fedha kwa kulipwa ruzuku katika awamu 16 ili kuziwezesha kuwekeza katika lishe, afya na elimu.
Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi unatekelezeka?
Waziri Kairuki alisema Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership) ulianza kutekelezwa nchini toka mwaka 2012/13, na umejikita katika kuweka uwazi zaidi katika uendeshaji wa shughuli za Serikali; Ushirikishwaji wa Sekta za Umma na Binafsi katika utekelezaji wa Mpango; Uwajibikaji wa Serikali kwa Wananchi; Matumizi ya Teknolojia na Ubunifu; na Mapambano dhidi ya Rushwa.
Alisema miongoni mwa yaliyofanyika ni pamoja na kuongezeka kwa uwazi kuhusu bajeti ya Serikali kwa kuandaa kijitabu cha  “Citizen budget” kilichoandaliwa kwa Kiswahili na  lugha rahisi kwa kuchapishwa kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha na Mipango. Pia, taarifa za utekelezaji za sekta za kipaumbele Afya, Elimu na Maji kuchapishwa katika Tovuti za sekta hizo na kukamilika kwa zoezi la upembuzi yakinifu wa Takwimu Huria (Open Data) ili  kuongeza uwazi wa takwimu na taarifa mbalimbali;
Waziri Kairuki alisisitiza kuwa Serikali inaendelea kutekeleza Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi kwa mikakati mbalimbali ikiwamo, kuendelea na utekelezaji wa kuwa na uwazi katika bajeti ya Serikali kwa kuweka taarifa za bajeti kwenye tovuti mbalimbali kwa lugha nyepesi na kwa Kiswahili na kuimarisha mfumo wa Takwimu Huria ambayo utarahisha wadau mbalimbali kupata takwimu zinazohusu masuala mbalimbali hususan Afya, na Elimu.
Majukumu ya Ofisi ni yapi?
Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora (OR-MUUUB) ina majukumu ya kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Sera za Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma; Taratibu, Miundo na Mifumo ya Utoaji Huduma; Uendelezaji Rasilimaliwatu; Utunzaji wa Kumbukumbu na Nyaraka katika Utumishi wa Umma. Aidha, Ofisi hii inasimamia maadili ya Watumishi na viongozi wa Umma; mapambano dhidi ya  rushwa; Mfuko wa Maendeleo ya Jamii; Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge; Mfuko wa Rais wa Kujitegemea; na Taasisi ya Uongozi.

0 maoni:

Chapisha Maoni