Wiki kadhaa zilizopita kuliripotiwa taarifa kuwa Mtanzania amepigwa risasi nchini Marekani na kupoteza maisha, aidha kumeripotiwa taarifa nyingine kuwa Mtanzania, Andrew Sanga amepigwa risasi Houston, Texas, Marekani.
Katika taarifa ambayo imetolewa na Msemaji wa HTC, Cassius Pambamaji imeeleza kuwa Sanga alipigwa risasi na watu wasiofahamika na kwa sasa Polisi wa nchini Marekani wanafanya uchunguzi kuhusu tukio hilo ili waweze kuwafahamu waliohusika katika tukio hilo.
Kwa upande wa msemaji wa familia, Prosper Kiswaga amesema kwa sasa Sanga yupo Hospitali ya Memorial Hermann Southwest, Houston, Texas katika Chumba cha Wagonjwa Mahututi (ICU) na hali yake bado sio nzuri.
Ameeleza kuwa kwa sasa anayeruhusiwa kumwona Sanga ni mke wake, Emmy Matatu na hivyo kuwaomba Watanzania kuungana na wanafamilia kwa ajili ya kumuombea ndugu Andrew Sanga ili aweze kurejea katika hali yake ya awali.