Jumatano, 20 Aprili 2016

NHIF yatoa msaada wa saruji tani tatu Mkoa wa Pwani


MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya umetoa msaada wa saruji tani tatu katika shule ya Sekondari ya Kilangalanga iliyopo mkoani Pwani kwa lengo la kujengea ukuta na kuimarisha hali ya usalama shuleni hapo.
Akikabidhi msaada huo, Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti Rehani Athumani alisema  kuwa Mfuko unatoa kipaumbele kikubwa katika suala la elimu kutokana na  kuwa na umuhimu mkubwa katika suala la afya.
“Jamii ikiwa na elimu au ikielimika hata baadhi ya magonjwa yataondoka  yenyewe…hivyo Menejimenti imeona ni vyema ikawaunga mkono katika suala hili ili hawa watoto wawe kwenye mikono salama na mazingira safi ya  kusomea,” alisema Rehani.
Aidha aliwataka wanafunzi wa shule hiyo kuhakikisha wanasoma kwa juhudi zote ili kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ya awamu ya Tano ambayo imetoa kipaumbele kikubwa katika suala la elimu.
“Nawaombeni sana tumieni muda wenu kwa kusoma vizuri na sio kufanya mambo ambayo yatawapotezea muda, Rais wetu wa Awamu ya Tano anapenda kila mmoja awe  na elimu bora hivyo tumieni hii fursa ili mje kuiongoza nchi badae,” aliwahamasisha wanafunzi hao.
Kwa upande wa Mjumbe wa Bodi wa shule hiyo Mbwana Chombiga akizungumzia msaada huo alisema kuwa kitendo kilichofanywa na NHIF ni cha kupigiwa mfano kwa kuwa shule hiyo imehangaika kwa kipindi kirefu bila kupata  msaada.
“Ndugu zangu kwa kweli sisi hatuna neno la kusema zaidi ya kuwashukuru tu…mnaona hata wanafunzi wana furaha kweli maana wanaona sasa mazingira yao yatakuwa bora, tunawashukuru sana na tunasema tutashirikiana nanyi katika elimu ya wananchi kujiunga na huduma za Mfuko,” alisema Bw. Chombiga.
Katika hatua nyingine Mfuko ulikubali ombi la shule hiyo la kuwa mlezi wa shule.
1 (1)Mkurugenzi wa Masoko na Utafiti Rehani Athumani akiwasalimia wanafunzi wa shule ya Sekondari Kilangalala Mkoani Pwani.
3 (2)Ofisa Masoko na Elimu kwa Umma Grace Michael akigawa vipeperushi vyenye ujumbe wa huduma ya Toto Afya Kadi kwa wanafunzi hao.2Sehemu ya Msaada wa Saruji tani tatu ukikabidhiwa kwa shule hiyo kwa lengo la kusaidia ujenzi wa uzio

0 maoni:

Chapisha Maoni