Jumatatu, 25 Aprili 2016

MIKOA YA IRINGA,NJOMBE,MBEYA YAONGOZA KWA MAAMBUKIZI YA VVU

MIKOA ya Njombe, Iringa na Mbeya imetajwa kuwa ndio mikoa yenye maambukizi makubwa zaidi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) nchini kutokana na kuwa na mwingiliano mkubwa wa watu unaosababishwa na shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Hayo yalisemwa jana na Mratibu wa Tume ya kudhibiti Ukimwi (Tacaids) Mkoa wa Mbeya, Edwin Mweleka, wakati alipokuwa Mgeni Rasmi kwenye utambulisho wa Mradi wa ushirikishaji wa wananchi wanaoishi na virusi vya Ukimwi wa ‘Sauti yetu’ unaofadhiriwa na wananchi wa Marekani kuipitia Shirika la USAID.

Mweleka alisema kuwa Mkoa wa Njombe ndio unaoongoza na kwamba maambukizi yamefikia asilimia 14.8, ukifuatiwa na Iringa wenye asilimia 9.1 na Mbeya unashika nafasi ya tatu ukiwa na asilimia 9, ambapo alisema kuwa mradi huo wa ‘Sauti yetu’ utasaidia kupunguza maambukizi hayo.

“Tunashukuru wenzetu wa Marekani kwa kutusaidia kufadhili Mradi huu wa Sauti yetu kupitia shirika lao la USAID, na naamini kwa mikoa yetu hii yenye maambukizi makubwa mradi huu utakuwa msaada mkubwa katika kupunguza maambukizi,” alisema.

“Mikoa ya ukanda wetu wa Nyanda za Juu Kusini ndiyo inayooongoza kwa maambukizi ikiongozwa na Njombe ambao ndio mkoa ambao unaongoza kitaifa wenye asilimia 14.8 ukifuatiwa na Iringa wenye asilimia9.1 huku Mbeya tukishika nafasi ya tatu kwa asilimia 9, hivyo kampeni itakayokuwa inaendeshwa kupitia ‘Sauti yetu’ tunatarajia itusaidie kupunguza maambukizi hayo mpaka kufikia Sifuri Tatu,” alisisitiza Mweleka.

Mweleka alisema kuwa mikoa ya Mbeya na Iringa haijawahi kutoka kwenye orodha ya mikoa mitatu yenye maambukizi makubwa tangu tafiti zilipoanza kufanyika katika miaka ya 2003/2004.

Mwenyekiti wa Baraza la Watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi Nchini, Justine Mwinuka, alisema kuwa mradi huo unatekelezwa katika Halmashauri 46 zilizopewa kipaumbele nchi nzima huku katika Mkoa wa Mbeya zikihusika Halmashauri tatu ambazo ni Mbeya Jiji, Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali.

Alisema kuwa watu wanaolengwa kwenye mradi huo ni wale wanaoishi na VVU pamoja na wenye TB kwa madai kuwa magonjwa hayo yana uhusiano wa moja kwa moja.

Alisema kuwa Mradi huu unatambulishwa kwa waratibu wa Ukimwi shughuli za Ukimwi ngazi ya Halmashauri pamoja na watendaji wa mabaraza ya watu wanaoishi na VVU Ngazi za Wilaya (Konga)

Kwa upande wake Meneja wa Mradi huo wa ‘Sauti Yetu’, Rachel Jacob, alisema kuwa changamoto inayowakumba watu wanaoishi na VVU kwa sasa ni unyanyapaa binafsi hali ambayo huwafanya watu hao kuishi kwa wasiwasi wakati wote.

Alisema lengo kubwa la mradi huo ni kutoa hamasa kwa jamii kupima afya zao kuanzia ngazi ya familia mpaka Taifa ili kila mtu aweze kuijua afya yake na wale wanaokutwa na maambukizi waweze kuanzishiwa dawa.

Jacob alisema kuwa Mradi huo ulianza kutekelezwa tangu mwezi Oktoba 2015 na utakamilika mwezi Oktoba mwaka 2019.

0 maoni:

Chapisha Maoni