MIEZI mitano tangu atoke madarakani, Rais
wa awamu ya nne, Dk Jakaya Kikwete amesema kwa sasa anafurahia maisha ya
uraiani na kwamba anajiandaa kuwa mzee mashuhuri nchini atakapokabidhi chama.
Akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya BBC,
Kikwete alisema maisha nje ya Ikulu ya Magogoni ni mazuri kwa sababu ametua
mzigo wa kuhudumia watu milioni 50 na kwamba sasa anaendelea na mambo yake
binafsi.
“Maisha baada ya kutoka madarakani ni
mazuri kwa sababu sina presha niliyokuwa nayo, nilikuwa na mzigo mkubwa wa
kuangalia taifa hili la watu milioni 50, siyo mzigo mdogo, ni kazi kubwa… Sasa
hivi unarudi nyumbani hauna faili, ninafanya mambo ninayoyapanga mimi, na
shughuli ninazofanya ni za kimataifa tu, niko kwenye hili la Libya (mjumbe wa
usuluhishi wa mgogoro wa Libya), naondoka karibuni, tuna mkutano Marekani wa
mambo ya malaria,” Kikwete aliiambia BBC.
Mbali na shughuli hizo, kwa sasa Kikwete
yupo kwenye Kamisheni ya Elimu na Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Gordon
Brown na pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
“Kuhusu siasa, bado ni Mwenyekiti wa CCM
na baada ya muda, nitakabidhi baada ya hapo kila kitu nitamuachia mzee Magufuli
aendelee nayo, mimi nitabaki ni mzee tu maarufu katika nchi yetu, maisha ni
mazuri tu,” alisema Kikwete.
Tangu alipoachia kiti cha urais na
kumkabidhi Dk. John Magufuli baada ya kuapishwa Novemba 5, mwaka jana, Kikwete
amekuwa akiishi nyumbani kwake Msoga mkoani Pwani baada ya kuhamia huko na
familia yake, Novemba 6, mwaka jana.
0 maoni:
Chapisha Maoni