Na Jacquiline Mrisho -MAELEZO
DAR ES SALAAM
Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imesema
kuwa makampuni binafsi ya ulinzi yanayofanya kazi bandarini hayahusiki
na ulinzi wa sehemu nyeti za za Mamlaka hiyo.
Akitoa ufafanuzi huo leo jijini Dar es
salaam, Meneja Mawasiliano wa Mamlaka hiyo Bi. Janeth Ruzangi amekiri
kuwepo kwa makampuni yanayofanya kazi ya ulinzi bandarini na amefafanua
kuwa hayahusiki kwa namna yoyote ile kulinda sehemu za ndani za ofisi
zilizoko bandarini.
“Ninapenda kuwafahamisha wananchi kuwa
Bandari inalindwa na walinzi wa aina tatu ; Jeshi la polisi, Polisi
wasaidizi walioajiriwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania (Auxilliary
Police) pamoja na walinzi wa Makampuni binafsi”
Ameongeza kuwa makampuni hayo yanalinda
maeneo ya nje ya bandari yakiwemo maegesho ya magari ya watumishi wa
mamlaka kama ilivyo kwenye ofisi nyingine.
Aidha,amefafanua kuwa Polisi wa bandari
walioajiriwa na Mamlaka ya Bandari Tanzania wako kwa mujibu wa sheria
zilizotungwa na Bunge na wamepata baadhi ya mafunzo ya kipolisi.
Ikumbukwe kuwa agizo la kuwandoa walinzi wa
makampuni binafsi kwenye maeneo nyeti ya bandari lilitolewa na Waziri
Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa mwezi Februari mwaka huu alipofanya ziara ya
kushtukiza bandarini hapo.
0 maoni:
Chapisha Maoni