Ijumaa, 28 Oktoba 2016

MUSWADA WA HABARI KUSAIDIA KUKUZA DIPLOMASIA YA UCHUMI

Posted by Esta Malibiche on Oct 28.2016 inNEWS

dkt-bernard-achiula-702x336

Dkt. Bernard Achiula:

Na. Immaculate Makilika- MAELEZO
Udhibiti  wa huduma ya habari  kwa namna ya ili  kulinda  usalama, utulivu amani na maslahi ya kiuchumi, maadili au afya ya jamii ni jambo jema  ambalo huzingatiwa na nchi zote duniani.
Hayo yamesemwa na Kaimu Mkuu wa Chuo cha Diplomasia, Dkt. Bernard Achiula  alipokuwa akifanya  mahojiano kuhusu namna muswada sheria ya huduma za habari unavyoweza kusaidia kukuza diplomasia ya uchumi nchini.
Dkt. Achiula  alisema kuwa vyombo  vya  habari vina jukumu kubwa la kulinda amani ya nchi  na kwa kuwekwa misingi ya uwajibikaji kwa waandishi wa habari itakayosaidia kulinda maslahi ya Taifa.
“Muswada huu upitishwe ili vyombo vya habari vifanyekazi katika misingi ya taaluma kwa kutoa taarifa  zenye  kweli kwa jamii, zitakazoitangaza nchi kimataifa ili kujenga diplomasia ya uchumi, itakayosaidia katika kulinda heshima utulivu na amani ya nchi”
“Muswada huu pia utasaidia waandishi wa habari kuandika habari zitakazoiletea sifa nchi na kuvutia watalii na wawekezaji  kwa kuzingatia amani iliyopo nchini, mbali na hapo diplomasia ya uchumi  itaweka mazingira rafiki katika kufikia azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Tanzania ya kufikia uchumi wa kati kupitia viwanda ifikapo mwaka 2020” alisema Dkt. Achiula
Sehemu hii ya muswada wa huduma za habari unaakisi mikataba ya kimataifa ikiwemo mkataba wa geneva ibara ya 19 inayoainisha haki wa wajibu kwa mwandishi wa habari hasa katika maeneo yanayohusu usalama, utulivu amani na maslahi ya kiuchumi, maadili au afya ya jamii.
Akizungumzia  kuhusu  Bodi ya Ithibati iliyopo katika muswada huo, Dkt. Achiula alisema kuwa Bodi hiyo itasaidia kukuza kanuni za maadili kwa wanahabari na kukuza weledi jambo litachochea mahusiano yenye faida katika nyanja za kimataifa.

Ameongeza kuwa kuwemo kwa  Baraza Huru la Habari kutasaidia  kuijengea uwezo sekta habari nchini kwa vile muswada huo utazalisha  waandishi wa habari  waliobobea katika fani mbalimbali, huku akitolea mfano nchi zilizoendelea ikiwemo Ujerumani kwa kuwa na chombo kinachosimamia masuala ya sekta ya habari  kwa kufuata misingi na utaratibu maalumu.
Aidha, wadau wa sekta ya habari nchini, wametakiwa kuendelea kutoa maoni yao ya kuboresha Muswada wa huduma za habari, kabla muswada huo  kusomwa tena bungeni ifikapo novemba mosi, mwaka huu.

0 maoni:

Chapisha Maoni