Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera na Uratibu Dkt.Hamisi Mwinyimvua amekutana na Kamati ya Taifa ya Uratibu wa Maafa kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali ya Menejimenti ya Maafa.
Mkutano huo ulifanyika Novemba 04, 2016 katika Ofisi ya Waziri Mkuu Dar es Salaam na kuhusisha wadau mbalimbali kutoka Wizara, Idara na Taasisi za umma zinazohusika na shughuli za maafa.
Dkt. Mwinyimvua alieleza kuwa katika kutimiza malengo ya Kamati hiyo, Ofisi ya Waziri Mkuu inajukumu la kuandaa mkutano wa Kamati ya Taifa wa Uratibu wa Maafa Nchini ili kukidhi matakwa ya kisheria.
“Ofisi ya Waziri Mkuu inawajibu wa kuratibu mkutano huo ili kuhakikisha unafanyika kwa mujibu wa sheria ya maafa namba 9 ya mwaka 1990 na inaelekeza kikao kiwe kinafanyika kila robo ya mwaka au pale inapotokea dharura/maafa yatakayolazimu kikao kufanyika,” alisema Dkt.Mwinyimvua
Miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na kupata taarifa za kukabiliana na maafa mbalimbali nchini, kuanzishwa kwa Wakala wa Usimamizi wa Maafa na kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasilano ya Dharura (Emergency Operation and Communication Center).
Vile vile Wajumbe wa mkutano huo walipata fursa ya kujadili masuala ya Menejimenti ya Maafa hususani katika masuala ya Mpango wa Taifa wa Ufuatiliaji na Uokoaji, taarifa za Hali ya Hewa nchini na kutoa maelekezo ya hatua za kuchukuliwa na wadau mbalimbali na wananchi kwa ujumla na kujadili Utekelezaji wa Mfumo wa kidunia wa Uboreshaji na Uimarishaji wa Utoaji na Matumizi ya Huduma za Hali ya Hewa.