Jumapili, 20 Novemba 2016

WAZIRI UMMY AENDESHA MKUTANO WA BARAZA LA KISEKTA LA MAWAZIRI WA AFYA WA NCHI ZA AFRIKA MASHARIKI

Posted by Esta Malibiche on Nov 20,2016 in NEWS 

ujim
Mhe Ummy akiongoza kikao cha Mawaziri wa Afya wa Afrika Mashariki. Kulia kwake ni Mhe Christophe Bazivamo Naibu Katibu Mkuu wa EAC…na kulia ni Dr Kwessi akimwakilisha Katibu Mkuu wa  Wizara ya Afya Tanzania
…………………………………………………………………
NA MWANDISHI WETU – NAIROBI 
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ameongoza kikao cha mkutano wa 13 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Afya wa nchi za Afrika Mashariki.
Mkutano huo ulifanyika juzi jijini Nairobi, Kenya ambapo pia ulijadili masuala mbalimbali yahusuyo sekta ya afya kwa ujumla.
Katika taarifa yake aliyoituma kwa vyombo vya habari, Waziri Ummy alisema mkutano huo ulihudhuriwa na Mawaziri wa Afya wa Kenya, Burundi, Uganda pamoja na Mwakilishi wa Waziri wa Afya wa Rwanda.
“Mkutano huo ulitanguliwa na kikao cha wataalam na kikao cha makatibu wakuu wa wizara za afya katika nchi wanachama vilifanyika kuanzia Novemba 14 hadi 17, mwaka huu,” alisema.
Alisema mambo makubwa yaliyojadiliwa na kupitishwa katika mkutano huo ni Sera ya Afya ya EAC (EAC Regional Health Policy) na Sera, Mwongozo na Mkakati wa EAC wa Afya ya Mama, Mtoto na Vijana (Intergrated EAC Reproductive, Maternal, Newborn, Child and Adolescent Health Policy Guidelines and Strategic Plan).
“Sera hizi zitasimamia utekelezaji wa mipango ya kuboresha na kuimarisha afya katika nchi wanachama wa Jumuiya kwa utaratibu unaofanana,” alisema.
Waziri Ummy alisema mkutano huo wa Mawaziri pia ulichambua na kupitia taarifa ya Makatibu Wakuu wa Wizara za Afya ambapo ulieleza kuridhishwa na hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa maagizo ya mawaziri wa afya ikiwemo kuanzishwa kwa mpango wa pamoja wa kusimamia dawa, mpango wa pamoja wa kukagua Vyuo Vikuu vya Afya pamoja na mpango wa pamoja wa huduma za UKIMWI/VVU. 
“Taarifa ya Ukaguzi wa Vyuo Vikuu vya Afya vya Tanzania itawasilishwa katika Kikao cha 14 cha Mawaziri wa Afya wa EAC kitakachofanyika Bujumbura Machi, mwakani,” alisema.
Aliwashukuru Mawaziri wa Afya wa Afrika Mashariki kwa kuendelea kusimamia vyema utekelezaji wa sera na mipango ya kuboresha na kuimarisha huduma za afya ktk nchi zao.
 Aliwataka kutekeleza maamuzi waliyokubaliana katika Mkutano huu ili kutimiza kwa vitendo matarajio ya wananchi wa Afrika Mashariki ya kuwa na Afya bora.
Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Kisekta la Afya la EAC hufanyika mara mbili kwa mwaka.
 Lengo la Mkutano huu ni kujadili utekelezaji wa sera, mipango na mikakati mbalimbali ya kuboresha huduma za afya kwa nchi za Afrika Mashariki

0 maoni:

Chapisha Maoni