Jumamosi, 12 Novemba 2016

Bustani za Mbogamboga zaiongezea kipato shule ya Msingi Mazoezi Bunda

Posted by Esta Malibiche on Nov 12,2016 in NEWS

ima
Na: Lilian Lundo – MAELEZO – MARA
Mradi wa bustani za mbogamboga katika shule ya Msingi Mazoezi Bunda iliyoko kata ya Nyasura, wilaya ya Bunda Mkoani Mara unaingizia shule hiyo kiasi cha shilingi 50,000 hadi 100,000 kwa kila mwezi.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Vicent Ndunguru aliyasema hayo Wilayani Bunda wakati wa mahojiano na timu ya wilaya inayosimamia mpango wa kuinua ubora wa elimu wilayani humo.
“Shule imeweza kujitunzia akiba ya fedha ambapo kabla ya mradi wa bustani za mbogamboga shule haikuwa na akiba yoyote lakini baada ya kuanzisha mradi huo, shule haikosi kuwa na akiba ya kiasi cha shilingi 50,000 mpaka 100,000 kwa mwezi,” alifafanua Mwalimu Ndunguru.
Mwalimu Ndunguru aliendelea kwa kusema kuwa, kutokana na mradi huo shule imeweza kujinunulia vifaa vya kufundishia kama vile chaki.
Pia fedha nyingine imekuwa ikitumika kutoa motisha kwa wanafunzi wanaofanya vizuri katika masomo pamoja na kutoa huduma ya kwanza  kwa mwanafunzi au mwalimu anayepata tatizo na kuhitaji matibabu ya haraka.
Aidha mradi huo umewajengea uwezo wa kujitegemea wanafunzi wa shule hiyo na kupelekea idadi kubwa ya wanafunzi wa darasa la sita kuanzisha bustani za mbogamboga majumbani kwao na kutumika kama chanzo cha mapato cha familia.
Mwalimu Ndunguru amewashauri walimu, kamati za shule na wazazi nchini kuwa wabunifu na kuanzisha miradi mbalimbali kama vyanzo vya mapato ambavyo vitasaidia kuendesha shughuli za elimu katika shule zao.

0 maoni:

Chapisha Maoni