Jumanne, 17 Mei 2016

Wakulima wawe makini na mvua hizi za masika.

indexNa Raymond Mushumbusi MAELEZO
Kwa miaka mingi hapa nchini Tanzania, Kilimo kimetajwa kuwa uti wa mgongo wa Taifa. Ikumbukwe kuwa miaka ya Sabini za mwanzoni kuliwahi kuwepo kauli kuhusu kilimo iliyosema “Kilimo cha Kufa na Kupona”. Kauli hii ililenga kuondoa njaa iliyokuwa inalikabili Taifa. Kwa miaka  ya hivi karibuni, serikali ikaja na Kauli Mbiu ya “Kilimo Kwanza”. Hizi zote ni jitihada za kuinua kilimo ambacho kinategemewa na walio wengi hapa kwetu.
Kilimo ni eneo la kipaumbele katika uchumi wa Tanzania licha ya kuwa  kilimo nchini bado kinategemea kwa kiasi kikubwa mvua na hali ya hewa kwa ujumla .
Kwa mujibu wa taarifa za mamlaka ya hali ya hewa iliyotolewa na  Mkurugenzi Mkuu Dkt. Agnes Kijazi zinasema mvua za masika zimeshaanza katika maeneo mengi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka. Mvua hizi zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani katika maeneo mengi. Hata hivyo maeneo machache yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani.
 
Hali ya unyevunyevu wa udongo inatarajiwa kuwa ya kutosheleza shughuli za kilimo katika maeneo mengi.Hata hivyo, mvua za juu ya wastani zinazoendelea kunyesha zinaweza kusababisha hali ya unyevunyevu wa udongo kupita kiasi hivyo kuathiri mazao na hata kusababisha mafuriko na kuharibu mazao.
 
 
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, msimu wa mvua za Masika katika kipindi cha miezi ya Machi hadi Mei, 2016 ni mahususi katika maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki (Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara), Pwani ya Kaskazini, (Mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Morogoro-Kaskazini pamoja na Visiwa vya Unguja na Pemba), Kanda ya Ziwa Victoria (Mikoa ya Kagera, Mara, Mwanza, Geita, Simiyu na Shinyanga) na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma. Mvua hizo zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani kwa maeneo mengi ya ukanda huo isipokuwa maeneo ya Kusini mwa ukanda huo yanatarajiwa kuwa na mvua za wastani hadi chini ya wastani.
 
Kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha tahadhari imetolewa kwa wakulima wote kuwa makini na mvua hizi za masika zinazoendelea kwani zinatarajiwa kunyesha kwa wingi katika baadhi ya maeneo kulingana na uelekeo wa upepo katika maeneo mengi ambayo yanayopata mvua za msimu wa masika.
 
Mwelekeo wa mvua uliotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa hivi karibuni umezingatia zaidi kipindi cha msimu(miezi mitatu) na hali ya mvua katika maeneo makubwa. Hivyo, viashiria vinavyochangia mwenendo wa mifumo ya mvua na mabadiliko ya muda mfupi katika maeneo madogo utazingatiwa katika uchambuzi wa utabiri wa muda wa kati na mfupi.
 
Wakulima wanashauriwa kuendelea na shughuli za kawaida za kilimo katika maeneo yao ikiwa ni pamoja na kutumia mbinu za kuongeza uzalishaji, kupanda mazao na miti kuzuia mmomonyoko wa udongo pamoja na kuzingatia ushauri wa wataalam wa kilimo katika matumizi sahihi ya ardhi na mbegu. Hata hivyo, katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za  chini ya wastani,upungufu wa unyevunyevu wa udongo unaweza kujitokea hususan katika vipindi vya kukosekana kwa mvua. Wakulima waendelee kutafuta, kupata na kuzingatia ushauri wa maafisa ugani katika kutekeleza shughuli zao.
 
Aidha wataalamu wa kilimo kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine(SUA) katika tafiti zao wametoa ushauri kuhusu namna bora ya kilimo cha baadhi ya mazao kwa kuzingatia taratibu sahihi za kilimo za mazao hayo wakati huu wa mvua za masika.

0 maoni:

Chapisha Maoni