Meya wa Jiji la Dare s Salaam
Mh. Issaya Mwita ameipongeza klabu ya Yanga kwa kunyakua ubingwa huo kwa
mara ya Ishirini na Sita tangu kuanzishwa kwa mashindano ya ligi kuu
hapa nchini.
Katika taarifa yake kwa vyombo
vya habari Mh. Mwita amesema ushindi wa Klabu ya Yanga umeliwezesha Jiji
la Dar es Salaam kuendelea kupata sifa katika medani ya Kitaifa na
Kimataifa kutokana na ushiriki wa klabu hiyo katika mashindano ya
kimataifa.
“Ninaiomba klabu ya Yanga
kuthamini ubingwa wao kwa kuonyesha viwango vya kimataifa ili kulifanya
jiji hili kuwa chuo cha mafunzo ya mchezo wa mpira wa miguu,” alisema
Mh. Mwita.
Aidha aliliomba Shirikisho la
Mchezo wa MPira wa Miguu nchini (TFF) kuendelea kusimamia ligi kwa
ustadi zaidi ili kulingana na taratibu za mpira wa miguu kama
zinavyoainishwa na Shirikisho la Soka duniani (FIFA) pamoja na
Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF).
“Naomba nitoe wito kwa wadau
wote katika familia ya mpira wa miguu kushirikiana ipasavyo ili kufanya
ligi yetu iwe miongoni mwa ligi bora barani afrika na Duniani kwa
ujumla,” aliongeza Mh. Mwita.
Pia aliwapongeza wadhamini wote
waliojitolea kusaidia ufadhili kwa vilabu vyote vilivyoshiriki ligi kuu
na kuwataka waendelee kuwasaidia ili kuinua soka letu la bongo.
Aidha ameitakia klabu ya Yanga
ya Jangwani maandalizi mema katika mchezo wa marudiano wa kufuzu hatua
za makundi ya kombe la Shirikisho la mpira wa miguu Barani Afrika (CAF)
dhidi ya klabu ya Sagrada Esperance huko nchini Angola.
0 maoni:
Chapisha Maoni