Jumatano, 25 Mei 2016

TANESCO yawataka wateja wake kuunganishiwa umeme na mafundi waliosajiliwa

TAN1Meneja wa Afya na Usalama kazini wa TANESCO, Mhandisi Majige  Mabulla.
………………………………………………………………………………………………..
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Shirika la Umeme Tanzania Nchini (TANESCO) limewataka wateja wake kuhakikisha wanaunganishiwa umeme na mafundi au wakandarasi waliosajiliwa na shirika hilo ili kupunguza ajali za moto.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Meneja wa Afya na Usalama kazini wa TANESCO, Mhandisi Majige  Mabulla alipokua akiongea na waandishi wa habari juu ya vyanzo vya ajali za moto vinavyosababishwa na umeme.
Mhandisi Mabulla alisema kuwa matukio ya moto yanayosababishwa na umeme hutokea kutokana na kuzalishwa kwa joto kali ndani ya nyaya kunakosababishwa na umeme kuwa mkubwa kuliko uwezo, kulegea kwa maungio ya nyaya pamoja na radi au nyaya za umeme kuangukia juu ya paa la nyumba.
Kwa mujibu wa Mhandisi Mabulla aliongeza kuwa ajali za moto zinazosababishwa na umeme huanza kama unavyoanza moto wa kiberiti au viwashio vinginevyo vya moto na husambaa haraka kwa kutegemea na aina ya vitu vilivyopo kwenye eneo husika kwa kuwa baadhi ya vitu hushika moto haraka na kuenea kwa kasi.
“Ajali za moto zinazosababishwa na umeme ni ngumu kutokea kama umeme utasukwa na mtaalam aliyebobea kwenye fani hiyo, TANESCO tunatoa wito kwa wateja wetu kuhakikisha wanafungiwa umeme na fundi au mkandarasi aliyesajiliwa na kampuni yetu,”alisema Mabulla.
Pia Mhandisi Mabulla alisema ili kuepukana na ajali za moto zinazotokana na hitilafu za umeme wateja wanapaswa ;kuepuka kupitisha nyaya za umeme juu ya paa za nyumba, kutokuunganisha umeme kutoka nyumba moja kwenda nyingine bila kupata maelekeza kutoka TANESCO.
Aidha Mhandisi Mabula alisema wateja pia wanapaswa kuhakikisha mfumo wa umeme unapitiwa upya kila baada ya miaka mitano pamoja na kuwa makini katika utumiaji wa vifaa vinavyotumia umeme kama vile pasi, hita za umeme.

TAN1Meneja wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi Kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mhandisi Majige Mabula akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) ambapo aliwataka wateja wa shirika hilo kuzingatia sheria na kanuni za matumizi ya umeme ili kuepuka ajali zinazoweza kusababishwa na hitilafu za umeme.Kulia ni Afisa Uhusiano wa Shirika hilo Bw. Yasini Silayo.
TAN2Baadhi ya Waandishi wahabari wakifuatilia mkutano huo. Picha na Hassan Silayo-MAELEZO
…………………………………………………………………………………………..
Frank Mvungi-Maelezo
Shirika la Umeme Tanzania limewataka wateja wake kuzingatia sheria na kanuni za matumizi ya umeme ili kuepuka ajali zinazoweza kusababishwa na hitilafu za umeme.
Kauli hiyo imetolewa leo Jijini Dar es salaam na Meneja wa Afya na Usalama kazini Mhandisi Majige  Mabulla wakati wa mkutano na vyombo vya habari.
Majige amesema kuwa moto hauwezi  kutokea endapo mtumiaji wa umeme atahakikisha kuwa mfumo wa umeme katika nyumba yake umesukwa na fundi ama mkandarasi aliyesajiliwa.
“Kuwa makini katika matumizi bora ya vifaa vinavyotumia umeme kama vile pasi,hita za umeme,kuchaji simu,kompyuta kutasaidia kupunguza au kuondoa tatizo la majanga ya moto” alisisitiza Mabulla.
Akizungumzia hatua nyingine zinazoweza kusaidia kuzuia majanga ya moto Mhandisi  Majige ni kuepuka kuweka vitu vinavyoweza kushika moto kirahisi karibu na nyaya ama maungio ya nyaya za umeme ndani ya nyumba .
Majige alitoa wito kwa watumiaji wa umeme kutoa taarifa pale wanapotaka kuongeza matumizi ya umeme kwa kiwango kikubwa ndani ya makazi ya watu ili tathmini ya uwezo wa nyaya kukidhi mahitaji yaliyoongezeka ifanyike.
Katika kuzuia matukio ya moto TANESCO imekuwa ikihakisha kuwa inamfikishia mteja umeme ulio salama na usiokuwa na madhara kwa mtumiaji kutoka kwenye nguzo mpaka kwenye mita.
Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwepo na matukio ya ajali za moto katika makazi ya watu ambayo yamekuwa yakisababisha madhara  ikiwemo kusababisha vifo,majeruhi  na uharibifu wa mali.

0 maoni:

Chapisha Maoni