Jumatatu, 16 Mei 2016

WAJUMBE WA KAMATI YA MISS TANZANIA 2016/17 WAIOMBA SERIKALI IWASAIDIE KUPATA WAFADHILI WA MASHINDANO HAYO

indexNa Mwandishi Maalum  – Dodoma
Wajumbe wa kamati ya Miss Tanzania 2016/17 wameiomba Serikali iwasaidie kupata wadhamini wa mashindano hayo kitaifa yanayotarajiwa kufanyika mwezi wa kumi mwaka huu.
Ombi hilo limetolewa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa kamati hiyo Hashim Lundenga wakati akiongea na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura alipokutana nao mjini Dodoma.
Lundenga alisema changamoto kubwa inayowakabili hivi sasa ni kupata ufadhili wa mashindano hayo ambayo yanafaida kwa mabinti wanaoshiriki hii ikiwa ni pamoja na kujengewa uwezo wa kuwa viongozi wazuri wa baadaye.
“Mwezi wa tisa warembo wanatarajiwa kuingia kambini watakaa huko kwa muda wa mwezi mmoja ambako watapewa mafunzo mbalimbali ikiwa ni pamoja kufundishwa jinsi ya  kujitambua na kujiendeleza kielimu”, alisema Lundenga.
Kwa upande wake Mhe. Wambura aliwapongeza wajumbe wa kamati hiyo kwa kuandaa mashindano hayo na kuwaahidi kushirikiana nao ili  kuhakikisha mashindano yanafanyika kama ilivyotarajiwa.
Mhe. Wambura alisema, “Nawapongeza washiriki wa mashindano haya walioiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Dunia kwani wameweza kushika nafasi nzuri katika mashindano ya makundi mbalimbali pia hawajawaangusha waandaaji wa mashindano kwa kuwa wanaendelea kuisaidia jamii inayowazunguka.
Naye Miss Tanzania,  Lilian Kamazima  alimshukuru Mhe. Naibu Waziri kwa kukubali kukutana nao na kusema kuwa mashindano hayo yanaumuhimu mkubwa lisha ya washiriki kupewa zawadi mbalimbali  lakini pia   wakiwa katika maandalizi ya mashindano  wanafundishwa jinsi ya kuwa wanawake wa kuigwa katika jamii, kuishi na kuisaidia jamii inayowazunguka.
Mashindano ya Miss Tanzania Taifa yanatarajiwa kufanyika mwezi wa kumi, hivi sasa mashindano ya vitongoji (Vituo) yanaendelea katika maeneo mbalimbali nchini baada ya hapo yatafuatiwa na mashindano ya Kanda.

0 maoni:

Chapisha Maoni