Jumatatu, 16 Mei 2016

Wanachama 950 wa Uzinza Saccos Bank Sengerema wakopeshwa milioni 60


sengNa Masanja Mabula-Sengerema
JUMLA  ya wanachama 950 wa Uzinza Saccos Bank iliyoko Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza  wamepatiwa mikopo yenye thamani ya  zaidi ya Shilingi milioni 60 katika kipindi cha mwaka 2015 .
Afisa mikopo wa Saccos hiyo Venus Mayengela ameyabainisha hayo huko  ofisini kwake Mjini Sengerema wakati akizungumza  na  mwandishi  wa habari hizi juu ya maendeleo yaliyofikiwa na Saccos  hiyo.
Alisema kati ya fedha hizo zaidi ya shilingi milioni 40  zimerejeshwa , na kuongeza kwamba wanachama waliokopeshwa fedha hizo wamo wakulima na wafanyabiashara ndogo  ndogo.
Hata hivyo alifahamisha kuwa pamoja na elimu inayotolewa na uongozi wa Saccos kuwataka wanachama kurejesha mikopo hiyo kwa wakati ,wapo baadhi ya wadaiwa sugu ambao wamekuwa wakikwamisha maendeleo ya Saccos .
“Tumeweza kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 60,685,000 kwa  wanachama wetu katika kipindi cha mwaka jana , lakini bado changamoto ya urejeshaji wa mikopo ni kikwazo cha maendeleo “alifahamisha .
Aidha alieleza kwamba  bado Saccos inadai zaidi ya shilingi milioni 26 ambazo ziko mikononi mwa wadaiwa sugu ambao wamezitumia fedha za mikopo kinyume na walivyokusudia .
Alisema ,kabla ya mwanachama kupewa mkopo uongozi wa Saccos unafanya ukaguzi wa awali kwa anayeomba mkopo ili kujiridhisha kwamba hakutakuwa na ugumu wa urejeshaji wake .
Akizungumzia hali za  maisha kwa wanachama waliokopeshwa alisema yamebadilika tofauti na walivyokuwa kabla wajajiunga na Saccos na kunufaika huduma zake .
“Maisha ya wanachama walionufaika na huduma za mikopo katika Saccos yetu zimebadilika na biashara zao wengi wao zinazidi kukua kila siku kutokana na kuongeza kwa mitaji yao pia “alieelza .
Hivyo aliwataka wanachama ambao bado wanadaiwa na Saccos kurejesha fedha hizo ili kutoa fursa kwa Uongozi kuweza kuwakopesha wanachama wengine .

0 maoni:

Chapisha Maoni