Jumanne, 17 Mei 2016

Kijiji cha Ishololo Halmashauri ya Shinyanga Vijijini wamuomba waziri Mwigulu Nchemba

index
Na Masanja Mabula –Shinyanga  
WAKAAZI  kijiji cha Ishololo Halmashauri ya Shinyanga Vijijini wamemuomba Waziri wa Kilimo , Mifugo na Uvuvi , Mwigulu Nchemba kufanya ziara ya kukagua ujenzi wa tuta la kuzuia maji ambalo limeanza kujengwa zaidi ya miaka 20 na limeshindwa kukamilika .
Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kijijini hapo walisema kwamba kuna harufu ya utumiaji mbaya wa fedha za ujenzi huo na kusema suluhisho pekee ni Waziri kufanya ziara kukagua maendeleo ya ujenzi huo .
Walisema ujenzi wa tuta hilo ulioanzishwa kwa nguvu za wananchi ambapo mwaka 2000 Serikali ilitoa shilingi milioni 35 , kufanikisha ujenzi huo ili kuimarisha kilimo cha mpunga kwa wakulima wanaozungukwa na mto huo.
“Hapa kuna majipu yanahitaji kutumbuliwa , hivyo tunamuomba Waziri Mwigulu Nchemba kututembelea na kukagua ujenzi wa tuta hili ambalo limeshindwa kukamilika huku serikali ikiwa imetoa fedha nyingi ”alisema Dotto Mayige .
Alifahamisha kuwa hata Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo alifika katika eneo hilo lakini anaonekana kushindwa kulipatia ufumbuzi tatizo hilo .
Aidha Sayi Mhoja alifahamisha pamoja na lengo zuri la kuanzisha ujenzi wa tuta hilo , bado limeshindwa kutumika kama lilivyokusudiwa na hivyo kuwafanya wakulima wa mpuga kutofikia malengo waliyojiwekea.
Alieleza , mkandarasi aliepewa kazi ya ujenzi wa tuta hilo ameodoka   na kuacha vifaa (magari) vikiwa vimetelekezwa huku wananchi wakipeana majukumu ya kuvilinda .
Aidha mwananchi mwengine aliyezungumza na mwandishi wa habari hizi ni Malale Juma ambaye alisema iwapo waziri atafanya ziara ya kukagua ujenzi huo , ataweza kusaidia wakulima wa mpunga kutatuliwa kwa kero zao .
“Kama hajaja Waziri hapa , ujenzi wa tuta hili hautakamilika kwani waliokabidhiwa kusimamia wanaonekana kujalia maslahi yao binafsi ”alieleza Malale.
Akizungumzia mavuno ya mpunga kwa msimu huu alisema baadhi ya wakulima wamepata hasara baada ya mvua ya mawe kunyesha na kuharibu mazao yao ambapo mavuno yameshuka kwa asilimia 98.
“Wapo baadhi ya wakulima ambao walikuwa wamepanga kuvuna magunia 10 , wamevuna debe moja , baada ya mvua kubwa iliyokuwa imeambatana na mawe kupukutisha mpunga ukiwa shambani ”alifahamisha.
Kukamilika kwa ujenzi wa tuta hilo kutawawezesha wakulima wa Mpunga kuendesha kilimo kwa njia ya umwagiliaji na hivyo kukabiliana na tatizo la njaa linaakabili.

0 maoni:

Chapisha Maoni