Jumamosi, 21 Mei 2016

SPIKA MSTAAFU MAKINDA AMPONGEZA MAGUFULI




SPIKA Mstaafu wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano Tanzania, Anne Makinda amesema kuchaguliwa kwa Dk John Magufuli kuwa Rais wa awamu ya tano kumewanusuru watanzania na machafuku yaliyokuwa yakielekea kutokea kwasababu ya tofauti kubwa ya vipato baina ya masikini na matajiri iliyokuwa ikiendelea kutokea.
Akizungumza na wanahabari kwenye mkutano uliokuwa unapitia utekelezaji wa program ya Ukanda  wa Kuendeleza Kilimo Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) katika kongani ya Ihemi inayohusisha mikoa ya Iringa na Njombe, Makinda alisema:
 “Tungeendelea tulivyokuwa tunaendelea, hakika tungekuja kuuana kwasababu wenye nacho waliendelea kupata zaidi na wasionacho waliongezeka kwa kuwa watumwa wa wenye nacho,” alisema.
Makinda alisema bahati mbaya iliyokuwa ikilikumba Taifa, baadhi ya matajiri ambao wengine hawaeleweki wanafanya kazi gani, walifikia mafanikio waliyonayo kutokana na ujanjaunja wa kunufaika kijanjajanja na fedha za serikali.
“Kuna watu walikuwa hawaeleweki wanafanya kazi gani, lakini ni mamilionea, baadhi yao ndio wale walikuwa wananufaika na mamilioni ya serikali,” alisema.
Akipongeza staili ya Dk Magufuli ya kuiweka nchi sawa katika Nyanja mbalimbali, Spika huyo mtaafu alisema kila mtanzania ataonja machungu yatakayokuja kuliponyesha taifa mbele ya safari.
Kutakuwa na magumu, wengi watasema aaha huyo bwana mbona kabana hivi, lakini ni muhimu watanzania wakajua hii ni oparesheni kubwa itakayotuumiza wote, lakini mwisho wa yote Taifa na watanzania tutapona,”alisema.
Makinda aliwataka watanzania waendelee kumuombea kwa Mungu, Dk Magufuli ili aendelee kuwa na afya njema, busara na afanye kazi kwa kasi aliyoanza nayo hadi atakapomaliza awamu yake ya kwanza ya miaka mitano.
Akizungumzia maisha yake binafsi baada ya kutoka kwenye siasa, alisema anajishughulisha na kilimo na akataja mazao mawili ya biashara anayolima kuwa ni pamoja na chai na mpunga.
Makinda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Chai alisema anafurahia kufanya kazi ya kuwatetea wakulima wa chai nchini na akaahidi kuhamasisha kwa nguvu zake zote uzalishaji zaidi wa zao hilo.

“Kama bodi ya chai, tunahamasisha uanzishaji wa viwanda katika maeneo yote yanayolimwa chai ili kuongeza tija katika kilimo hicho,” alisema na kutaja maeneo hayo kuwa ni pamoja na Njombe, Kilolo na Tarime.

0 maoni:

Chapisha Maoni