Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads)
mkoa wa Iringa imeanza kupanda miti katika maeneo ya hifadhi ya barabara za
lami mkoani hapa katika shughuli iliyozinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa,
Amina Masenza juzi.
Wakianzia Kihesa Kilolo, mjini Iringa
watumishi wa Tanroads na wadau wao wa barabara walipanda miti kwenye eneo lenye
urefu wa kilomita 2.8 katika hifadhi ya barabara ya Iringa Dodoma.
Meneja wa Tanroads mkoa wa Iringa, Mhandisi
Daniel Kindole alisema zoezi la upandaji miti litakuwa endelevu likilenga
kutunza mazingira katika hifadhi ya barabara katika maeneo yote yenye barabara
za lami zilizokamilika.
“Tumeanza na eneo hili la Kihesa Kilolo
katika kipindi hiki cha kiangazi kwasababu liko jirani na vyanzo vya maji,”
alisema na kuongeza kwamba kazi kubwa ya upandaji miti katika barabara hizo
utaendelea kwa nguvu kubwa wakati wa masika.
Alisema hifadhi ya barabara ni eneo
lililopembezoni mwa barabara kila upande ambalo limetengwa na kuwekwa kisheria
lengo kuu likiwa ni kwa ajili ya upanuzi, ujenzi au kwa matumizi wakati wa
matengenezo ya barabara.
Akizindua zoezi hilo, Mkuu wa Mkoa
alisema suala la kutunza mazingira ni suala la kila mtu lenye manufaa makubwa
kwa watanzania.
“Niwapongeze Tanroads kwa kuja na wazo
hili litakaroboesha mazingira na kusaidia kulinda hifadhi ya barabara isivamiwe
kwa shughuli zingine,” alisema.
Pamoja na kupanda miti alisema mazingira
ya barabara yanapaswa kutunzwa kwa kuzingatia sheria ya barabara Na 13 ya mwaka
2007 pamoja na kanuni zake za mwaka 2009 zinazozuia kufanya kazi za gereji, kutupa
taka ovyo, kuwasha moto, kukata miti, kulima na kuchimba mchanga au kokoto.
Mwenyekiti wa Kikundi cha Kutunza Mazingira Kihesa Kilolo (KIUMAKI) kilichopewa kazi ya kuimwagilia miti hiyo mpaka kipindi cha masika, Mbonea Ngwinzila alisema kwa kupitia makubaliano yao na Tanroads watahakikisha miti iliyopandwa katika eneo hilo inatunzwa.
0 maoni:
Chapisha Maoni