Alhamisi, 30 Juni 2016

SUGU, KUBENEA WASIMAMISHWA KUHUDHURIA VIKAO VYA BUNGE



Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi amesimamishwa kutohudhuria vikao 10 vya Bunge la 11 baada ya kupatikana na hatia kwa kosa la kuwaonyesha wabunge kidole cha kati wakati akitoka katika ukumbi wa Bunge.
Akisoma taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge iliyosikiliza na kuchunguza kesi hiyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo, George Mkuchika amesema wamemkuta mbunge huyo na hatia baada ya kumuhoji na kuangalia picha za video pamoja na ushahidi uliotolewa na baadhi ya wabunge walioona tukio hilo.
Bunge limeridhia Mbilinyi kupewa adhabu hiyo iliyopendekezwa na kamati.
Aidha, Naibu Spika, Dkt Tulia Ackson amewasimamisha wabunge wawili; Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea na Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya, wote kutoka CHADEMA kuhudhuria vikao vitano vya bunge kuanzia kikao cha leo kutokana na kusema uongo bungeni.
Kubenea amesimamishwa baada ya kubainika kusema uongo kwamba waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt Hussein Mwinyi kuwa ameingia Mkataba na kampuni ya China Henan International Cooperation Group Company wa ujenzi wa nyumba za JWTZ na nyumba ya Waziri huyo jambo ambalo sio kweli.

Naye Ole Millya amesimamishwa baada ya kushindwa kuthibitisha ‘ushemeji’ uliopo baina ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu , Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama na mmoja wa viongozi wa Sky Associate, inayomiliki mgodi wa Tanzanite One, Asia Gonga aliyeolewa na Yusuph Mhagama ambaye kwa mujibu wa Millya ni ndugu wa waziri huyo.

0 maoni:

Chapisha Maoni