Jumatatu, 27 Juni 2016

Sekta binafsi ishirikishwe katika utekelezaji wa Mpango

2Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri akizungumza wakati wa kufunga mkutano wa Wachumi na Maafisa Mipango uliofanyika katika ukumbi wa Hazina, Dodoma.
SONY DSC
………………………………………………………………………………………………
Na Joyce Mkinga
SEKTA Binafsi katika ngazi zote ni lazima ishirikishwa katika utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo 2016/17 – 2020/21 uliozinduliwa hivi karibuni.
Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Bibi Florence Mwanri aliyasema hayo alipokuwa akifunga mkutano wa Wachumi na Maafisa Mipango uliofanyika mjini Dodoma mwishoni mwa wiki.
Bibi Florence Mwanri amesema sekta binafsi ni wadau muhimu katika utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo hivyo, wanatakiwa kushirikishwa katika mipango yote ya Serikali.
“Katika mipango yetu katika ngazi zote lazima sekta binafsi ishirikishwe kwa sababu wao ndio watekelezaji wakubwa wa mpango huo” alisema Bibi Mwanri
Amesema maafisa mipango wanapoibu miradi mbalimbali katika ngazi ya kijiji, wilaya, mkoa ni lazima sekta binafsi ishirikishwe ili kuwapa fursa nzuri ya kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo ambao unalenga katika Kujenga Uchumi wa Viwanda ili Kuchochea Mageuzi ya Kiuchumi na Maendeleo ya watu
Mkutano huo uliwashirikisha wachumi na maafisa mipango 170 kutoka katika wizara, idara za serikali, sekretarieti na mikoa na wilaya, taasisi za utafiti, na sekta binafsi ulikuwa na kaulimbiu ya Kuelekea kwenye Utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo 2016/17 – 2020/21.
Lengo kuu la Mkutano huo ilikuwa ni kujenga uelewa wa pamoja juu ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano na utelekezaji wake.
Mpango huo unatarajia kugharimu Trilioni 107 ambapo Sekta binafsi itachangia  Trilioni 48.
Akiwasilisha maazimio ya mkutano huo Kaimu Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango kutoka Klasta ya Uchumi Jumla, Dkt. Lorah Madete amesema Serikali na sekta binafsi wakutane pamoja na kupanga mikakati ya kutekeleza mpango huo wa maendeleo.
Vile vile, Dkt Madete alisema kuwa kuna haja ya Serikali kuingiza Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Dunia katika mipango ya Serikali ikiwa ni pamoja na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano.
Mkutano huo uliandaliawa Tume ya Mipango kwa ushirikiano na Taasisi ya Uongozi.

0 maoni:

Chapisha Maoni