Jumamosi, 25 Juni 2016

PELUM TANZANIA YATOA MAFUNZO YA HAKI ZA ARDHI MKOANI IRINGA





WAJUMBE wa kamati za uamuzi za vijiji 10 vya wilaya za kilolo na Mufindi mkoani Iringa wamepata mafunzo ya haki za ardhi na utawala yatakayowaongezea uelewa juu ya sheria za ardhi, haki za ardhi kwa wanawake na makundi maalum pamoja na utatuzi wa migogoro ya ardhi.
Mafunzo hayo yaliyofanywa kwa siku nne katika kila wilaya yametolewa na mtandao wa Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali yanayofanya kazi na wakulima na wafugaji wadogo nchini Tanzania (PELUM Tanzania).
Afisa Mradi wa PELUM Tanzania, Angolile Rayson alivitaja vijiji hivyo kuwa ni pamoja na Ikuka, Mbigili, Mawala, Mawambala na Masalali kwa upande wa wilaya ya Kilolo na  Isaula, Magunguli, Makungu, Usokami na Ugesa kwa upande wa wilaya ya Mufindi.
Alisema mafunzo hayo yanatolewa kupitia mradi wa kuhusisha jamii ya vijijini katika uwajibikaji wa masuala ya ardhi ya kijiji unaojulikana kwa jina la CEGO unaotekelezwa kwa uratibu wa mtandao huo na ufadhili kutoka shirika la kimataifa la maendeleo la Marekani (USAID).
Rayson alisema mradi huo wa miaka minne ulianza kutekelezwa mwaka 2013 ukihusisha pia vijiji vingine 20 vya wilaya nne katika mikoa ya Morogro na Dodoma.
“Shughuli kuu za mradi huo ni kuongeza na kuimarisha uelewa wa haki za ardhi kwa wananchi wa vijijini pamoja na viongozi wao kupitia mafunzo, machapisho  na mijadala mbalimbali,” alisema.
Alisema lengo likiwa ni kuhakikisha kunakuwepo na matumizi mazuri na endelevu ya ardhi ya kijiji kwa ajili ya uhakika wa chakula na kipato kwa wananchi.
Akifunga mafunzo hayo wilayani Mufindi juzi, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Isaya Mbenje alisema ardhi ni mojawapo ya rasimilali muhimu sana kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika nchi.
“Hivyo ni muhimu kwa jamii yetu kuwa na uelewa wa kutosha juu ya sera na sheria za ardhi ili ardhi ya Tanzania itumike kwa manufaa ya watanzania wote na kwa usawa,” alisema. 
Akiishukuru PELUM Tanzania kwa kuleta mradi huo mkoani Iringa, Mbenje ili matumizi yake yawe endelevu ni muhimu wananchi vijijini wakaijua Sheria ya ardhi namba 4 na 5 ya mwaka 1999.
“Na ni muhimu uelewa wa viongozi juu ya majukumu yao katika usimamizi wa ardhi ya kijiji, na utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa njia ya amani pasipo kuvunja mahusiano mazuri baina ya watumiaji wa ardhi ukaongezeka,” alisema.
Awali mmoja wawashiriki wa mafunzo hayo, Festo Katingasa wa kijiji cha Usokami, Mufindi alisema mafunzo ya matumizi bora ya ardhi waliyopata kupitia mradi huo atayatumia kusaidia utatuzi wa migogoro ya ardhi katika kijiji chake.
“Chanzo cha migogoro mingi ya ardhi katika kijiji chetu ni ukosefu wa hati miliki za ardhi inayoonesha mipaka aya ardhi kwa matumizi mbalimbali,” alisema.
Naye Salima Nyato wa kijiji cha Magunguli alisema kwa miaka mingi wanawake wamekuwa wakikosa haki ya kumiliki ardhi na kwamba mafunzo hayo yatawasaidia kuipata haki hiyo.

0 maoni:

Chapisha Maoni