HALMASHAURI ya wilaya ya Kilolo mkoani
Iringa imeitisha baraza maalumu la madiwani, Julai 17 mwaka huu, litakalojadili
hatma ya mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Rukia Muwango anayeendelea na majukumu
yake pamoja na kusimamishwa kazi na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI),
George Simbachawene.
Muwango alisimamishwa kuendelea kuwa
mkurugenzi wa halmashauri hiyo pamoja na wakurugenzi wengine wanne wa
halmashauri za Tunduma, Nanyumbu, Mbogwe na Misenyi kupitia taarifa ya waziri
huyo aliyoitoa Februari 17, mwaka huu wakati akizungumza na wanahabari.
Kwa kupitia taarifa yake hiyo,
Simbachawene alisema wakurugenzi hao walikuwa wakishawishi kutoa rushwa kwa
maofisa wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ili watoe
hati safi licha ya kubainika kuwepo kwa kasoro katika halmashauri zao
Wakizungumza na wanahabari juzi mjini
Kilolo, madiwani hao walisema Mei 7 mwaka huu waliamua kuomba baraza hilo
maalumu kwa kuzingatia taratibu zinavyotaka na kuwasilisha kwa mwenyekiti wa
halmashauri hiyo.
Diwani wa Kata ya Ruaha Mbuyuni, Issa Mwisomba alisema; “tunataka baraza hilo ili tuelezwe kwanini waziri alitangaza kumsimamisha mkurugenzi wetu na kwanini hakubatilisha kauli yake maana mkurugenzi huyo anaendelea na kazi zake kama kawaida.”
0 maoni:
Chapisha Maoni