Jumatano, 29 Juni 2016

Bunge limepitisha muswada wa marekebisha ya sheria ya ununuzi wa umma wa mwaka 2016

3Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
——————–
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo limepitisha muswada wa marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma wa Mwaka 2016 wenye lengo la kupunguza gharama na muda wa mchakato wa manunuzi Serikalini.
Marekebisho hayo yametokana na gharama kubwa ambayo Serikali imekuwa ikitumia kutokana na huduma na Bidhaa zinazonunuliwa na Serikali kuwa za juu ikilinganishwa na bei ya wastani ya soko.
“Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Ununuzi wa Umma wa mwaka 2016 una lengo la kuongeza ufanisi katika ununuzi wa Umma kwa kuondoa mapungufu yaliyopo katika Sheria ya sasa kwa kupunguza gharama na muda wa michakato ya ununuzi, kutoa upendeleo kwa kampuni za ndani, vikundi maalum, malighafi na bidhaa zinazozalishwa nchini pamoja na kuweka viwango mahsusi kwa bidhaa zitakazotumiwa na Serikali,” alifafanua Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju.
Mhe. Masaju ameendelea kwa kusema kuwa sheria hiyo imeweka kifungu cha dharura  ili kuwezesha vitu vya kuokoa uhai na vinginevyo kununuliwa kwa dharura pindi inapobidi.
Kwa upande wake Mbunge wa Babati Vijijini Mhe. Jitu Soni yeye ameiomba Serikali kuruhusu kununua vifaa tiba vilivyotumika ambavyo muda wake wa kutumia hauna mwisho, kwa mfano vitanda vya kujifungulia  ili kupunguza gharama ya kununua vitanda vipya na kuweza kununua vitanda vingi kwa wakati mmoja.
Aidha Mhe. Jitu ameiomba Serikali kuirudisha tena Sheria hiyo Bungeni baada ya mwaka mmoja ili kufanyiwa marekebisho na kuziba mianya yote ambayo itakuwa imebainika mara baada ya utekelezaji wake kuanza.
Muswada wa marekebisho ya sheria hiyo yanasubiri kusainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli ili kuanza utekelezaji wake.

0 maoni:

Chapisha Maoni