Alhamisi, 9 Juni 2016

KIBAHA WALIA UKOSEFU WA MAJI SAFI NA SALAMA

K



Wananchi wa Mtaa wa Mwambisi wakifua kwa kutumia maji ya mabondeni


Wakazi wa Mtaa wa Mwambisi Kata ya Kongowe iliyopo wilayani wakichota maji ya mabondeni kutokana na maji safi na salama katika kata hiyo kutoka mara moja kwa wiki na kusababisha kero na hofu kwa watumiaji wa maji hayo. Picha zote na Elisa Shunda


Mmiliki wa Blog ya Shunda Blog,Elisa Shunda, akichota maji kwa ajili ya matumizi ya kuoga


Wananchi wa mtaa huo wakielekea katika eneo la Bonde la Miti Mirefu kuchota maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani kama kufulia nguo,kupikia na kunywa jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa afya yao.





NA ELISA SHUNDA,KIBAHA
Serikali imeombwa kuingilia kati suala la ukosefu wa upatikanaji wa maji safi katika kata ya Kongowe eneo la Mwambisi ambalo maji yamekuwa yakitoka mara moja kwa wiki na kusababisha wananchi kutumia maji ya mabondeni yasiyo salama kwa matumizi ya binadamu.


Wakizungumza na Raia Tanzania,jana wakazi wa maeneo mbalimbali wa kata hiyo walisema kuwa kutokana na kutopatikana kwa maji safi na salama kwa wakati timilifu imepelekea watoto wananchi kuwa na mashaka na afya zao kwa kuhofia kupata magonjwa mbalimbali kama kuhara,kuumwa matumbo na kichocho.


Akichangia hoja hiyo mkazi wa mtaa wa Mwambisi,Maria Nicoulas alisema kuwa kutokupatikana kwa maji safi katika eneo la mwambisi ni kero kubwa sana kwa akina mama ambao muda mwingi wanautumia kusubiri maji mabondeni na pia maji yenyewe siyo salama kwa matumizi ya nyumbani lakini pia inaweza ikagombanisha familia kati ya baba na mama kwa kuingiza hisia tofauti kwa kuwa unaweza ukakaa kusubiri uchote maji hata masaa matatu.


“Sisi akina mama tunapata shida sana kupata maji kwa kuwa hata sehemu tunapoenda kuchota maji ni mbali na nyumbani na pia maji yenyewe huko kwenye mabonde ya mpunga ni mbali inachukua muda mwingi hadi kuludi nyumbani kwa hali kama hii inaweza kusababisha ugomvi kati ya baba na mama kwa kuingiza suala la wivu wa kimapenzi kumbe masikini ni kutokana na umbali wa sehemu tunapochota maji na foleni iliyopo hivyo tunaiomba serikali iangalie kuhusu tatizo hili”Alisema Maria

Mkazi wa Bamba, Juma Abdul,alisema kuwa kutokana kukatika mara kwa mara kwa maji katika maeneo mbalimbali ya kata hiyo imekuwa ni kero na usumbufu kwa wananchi ambapo huwaletea kutumia fedha nyingine ya ziada kununua maji safi wakati mabomba yapo lakini hayatoi maji.


Aidha wananchi hao wananchi hao wameiomba serikali kutoa msaada wa hali na mali kuhakikisha huduma hiyo muhimu inarejea kama hapo awali ili kuondoa uwezekano wa kutokea milipuko ya magonjwa ya matumbo na kichocho.


Akichangia kuhusu kero hiyo Aliyekuwa mgombea Udiwani wa kata hiyo kupitia Chama cha Wananchi (Cuf),Mathas Kambi,alisema kuwa suala la maji safi na salama kwenye kata ya kongowe ni tatizo sugu sana,linatokana na sababu kuu zifuatazo kwanza viongozi wa kata pamoja na viongozi wa serikali za mitaa kutotambua ufuatiliaji wa kero hiyo, pili dawasco wenyewe pia hawako sawa kwenye huduma zao, kwa maana miundombinu yao kwenye usambazaji haipo sawa.


“bomba kubwa linaweza kuharibika visiga wiki nzima watu wa kongowe tunaweza kukosa maji kutokana na tatizo hili afadhali ya mwambisi na Bamba maeneo ya kwamwami upande wa kulia kama unaenda mlandizi kule hawajui maji tokea kongowe imefahamika eneo la bamba upande wa kushoto kuna watu wamechangishwa pesa na mwenyekiti wao Mavala mamilion ya pesa mpaka leo maji hakuna ni utapeli mtupu , miembe saba B toka imezaliwa mpaka leo hawajui lini watapata maji safi na salama ,huko mwambisi ndiko tatizo kama linavyojionyesha”Alisema Kambi


Akizungumza kuhusu suala hilo Diwani wa Kata ya Kongowe,Iddi Kanyalu,alisema kuwa tatizo hilo limefika ofisini kwake na kusema kuna shida ya kukatika kwa maji sana katika eneo la Mwambisi na Vikunai na ameshalipeleka katika ofisi za Shirika la majisafi na majitaka Dar es salaam (DAWASCO) wilaya ya Kibaha alisema uongozi wa shirika hilo wamemuambia kuwa tatizo kubwa ni baadhi ya wananchi wanajiunganishia mabomba kiholela na muda si mrefu wataanza kufanya oparesheni katika makazi ya watu.


“Nimepata taarifa za kuwepo kwa shida ya maji katika maeneo mbalimbali ya kata yangu ya Kongowe nimefikisha kwa uongozi wa Dawasco ambapo wameniambia kutokea kwa hali ya kukatika maji sababu kubwa ni baadhi ya wananchi ambao si waaminifu wamejiunganishia mabomba kinyume na sheria hali inayosababisha ukosefu wa maji na pia uongozi umeniambia kuanzia wiki hii wanaanza oparesheni ya kupitia katika makazi ya watu ili kubaini watu waliojiunganishia maji kiholela”Alisema Kanyalu

0 maoni:

Chapisha Maoni