Jumamosi, 25 Juni 2016

UN yazindua sehemu ya pili Mpango wa Misaada ya Maendeleo (UNDAP 2)

Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Alvaro Rodriguez akizungumza katika halfa ya kuzindua mpango wa misaada ya maendeleo UNDAP 2 2016-2021.
 
Katika kuendeleza juhudi zake za kusaidia mataifa wanachama, Umoja wa Mataifa (UN) umezindua mpango mpya wa misaada ya maendeleo nchini (UNDAP 2) baada ya mpango wa kwanza wa UNDAP 1 kukamilika kwa mafanikio makubwa na hivyo kuzinduliwa mpango mpya ambao utaendeleza hatua uliyoishia mpango wa kwanza.
Katika mpango huu mpya UN inataraji kutoa kiasi cha Dola Bilioni 1.3 ambazo zitatumika katika kuboresha kusaidia kukuza uchumi na upatikanaji wa ajira, kuboresha huduma zinazopatikana katika sekta ya afya, kuboresha demokrasia, usawa wa kijinsia na haki za binadamu na kusaidia kupambana na mabadiliko ya tabia ya nchini.
Akizungumza katika halfa ya kuzindua mpango huo, Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Alvaro Rodriguez alisema utekelezaji wa mpango mpya wa UNDAP 2 utakwenda pamoja na utekeleji na Malengo ya Maendeleo Endelevu Duniani (SDGs).
Alisema kuwa Umoja wa Mataifa utaendelea kushirikiana na Tanzania katika kusaidia upatikanaji wa huduma bora za kijamii na ni matumaini yake kuwa wataendelea kudumisha ushirikiano uliopo sasa katika ya UN na serikali ya Tanzania.
“Mpango huu utaweka mbele vipaumbele vya taifa na utahakikisha kuwa hakuna mtu ambaye anaachwa nyuma ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo Endelevu ambao unataka kila mtu ahusike,
“Umoja wa Mataifa utaendelea kudumisha ushirikiano uliopo baina yake na Tanzania na itaendelea kuisaidia Tanzania pamoja na wananchi wake,” alisema Rodriguez.
Nae mgeni rasmi katika halfa hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Sheria na Katiba, Prof. Sifuni Mchome, alisema kuwa mpango huo umekuwa na matokeo mazuri kwa Watanzania lakini pamoja na hilo pia serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali zitakazoweza kukuza uchumi wa nchi na wananchi wake.
Prof. Mchome alisema kuwa serikali ya Tanzania inaushukuru Umoja wa Mataiffa kwa kuwaletea mpango wa pili baada ya awali kumalizika lakini pia serikali itahakikisha kuwa mpango huo utahusika kwa kila Mtanzania ili na yeye aweze kufaidika na mpango wa UNDAP 2.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Sheria na Katiba, Prof. Sifuni Mchome akizungumza kwa niaba ya serikali katika uzinduzi wa UNDAP 2.
 
“Tunashukuru baada ya ule wa kwanza mmetuletea mpango wa pili lakini pia hata pesa imeongezeka kwa sasa kupata Dola Bilioni 1.3 kutoka ule wa kwanza ambao ulikuwa wa Dola Bilioni 0.8 na katika mpango huu tutamshirikisha kila mwananchi na yeye afaidike nao,
“Serikali imekuwa ikifanya jitihada za kuleta maendeleo ya taifa na kwa mwananchi mmoja mmoja lakini bado tunawahitaji wadau kama nyie na tunawaomba msiondoke na tuendelee kufAnya kazi kwa kushirikiana,” alisema Prof. Mchome.
Mpango mpya wa misaada ya kimaendeleo ambao umetolewa na Umoja wa Mataifa (UN) unataraji kuanza Julai, 2016 na kumalizika Juni, 2021.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Job Masima akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dk. Juma Malik Akil akielezea jinsi UNDAP 1 ilivyosaidia sekta ya afya Zanzibar.

0 maoni:

Chapisha Maoni