Mamlaka
ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa mwelekeo wa hali ya
hewa kwa kipindi cha Juni hadi Agosti mwaka huu. Akizungumzia utabiri
huo kwa mbo vya Habari mapema leo Jijini Dar es Salaam kuhusiana na
mwelekeo huo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Meneja Kituo Kikuu cha
Utabiri Bw. Samwel Mbuya alisema Tanzania inatarajia kuwa na hali ya
baridi na vipindi vya mvua kwa maeneo machache ya nchi.
“Nchi
yetu inatarajia kuwa na hali ya baridi kiasi katika kipindi hiki
sambamba na vipindi vifupi vya mvua vinavyotarajiwa kujitokeza katika
maeneo machache hususan ya ukanda wa Ziwa Viktoria na ukanda wa pwani ya
Kaskazini (Visiwa vya Unguja na Pemba). Katika kipindi cha mwezi Juni
hadi Agosti 2016, maeneo mengi ya nchi yanarajiwa kuwa makavu na yenye
hali ya baridi kiasi katika majira haya ya kipupwe. ” alieleza Samweli Mbuya.
Meneja
huyo ameongeza kuwa mifumo ya hali ya hewa inaonesha matarajio ya hali
ya joto la wastani hadi chini ya wastani katika maeneo yaliyopo
Kusini-Magharibi mwa nchi.
Hata hivyo, katika msimu wa Kipupwe wa mwaka huu maeneo mengi ya nchi yanatarajiwa kuwa na joto la wastani hadi juu ya wastani.
Meneja huyo amebainisha kuwa, hali ya ubaridi inatarajiwa zaidi nyakati za usiku hadi mapema asubuhi. “Aliendelea
kueleza sababu za hali hiyo kuwa ni pamoja na kupungua kwa joto la
bahari katika eneo la ukanda wa Tropiki la bahari ya Pasifiki sambamba
na Joto la baharí katika eneo la magharibi wa bahari ya Hindi kuwa la
wastani kwa kipindi cha miezi ya Juni hadi Agosti 2016.
Aidha,
joto katika bahari ya Atlantiki linatarajiwa kuwa chini ya wastani.
Hali hiyo inatarajiwa kusababisha upepo kuvuma kutoka magharibi
ukielekea mashariki hususan katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Viktoria.
Joto la bahari la juu ya wastani linatarajiwa katika eneo la ncha ya
kusini ya bara la Afrika hivyo kuathiri msukumo wa upepo wa kusi.
Kwa
upande wake, Afisa Uhusiano wa TMA, Bi. Monica Mutoni alitoa msisitizo
kwa wananchi kufuatilia taarifa hususan za tahadhari zinazotolewa na
Mamlaka kupitia vyombo mbalimbali vya habari, tovuti ya Mamlaka na
vyanzo vingine vya habari ili kuokoa maisha na mali.
Bi.
Monica aliongeza kuwa: “Hivi karibuni TMA imekuwa ikitoa tahadhari
mbalimbali ikiwa ni pamoja na za kuwepo kwa upepo mkali na mawimbi
makubwa kwenye ukanda wa Bahari Hindi, Maziwa na nchi kavu hivyo ni
vyema wananchi hasa wale watumiaji wa bahari na maziwa kuchukua hatua
stahiki pindi taarifa kama hizo zinapotolewa”.
Aidha,
TMA ilipongeza sekta mbalimbali pamoja na Taasisi, Mamlaka za Serikali
na jamii kwa ujumla kwa hatua stahiki zilizochukuliwa katika kipindi
cha msimu wa mvua za Masika 2016 kwa kutumia Taarifa, Agalizo
na Tahadhari za utabiri zilizotolewa na Mamlaka. Ni wazi kuwa kwa hatua
hizo madhara ambayo yangeweza kujitokeza yalidhibitiwa na hivyo
kuchangia katika kufanikisha mipango na utekelezaji wa shuguli za
kiuchumi na kijamii katika kipindi husika.
Hata hivyo, TMA inahimiza wananchi kutembelea kwenye tovuti ya TMA www.meteo.go.tz ama ofisi zao popote zilipo ili kupata taarifa kwa kina kuhusiana na mwelekeo wa hali ya hewa kwa kila mkoa.
Tazama MO tv, kuona tukio hilo hapa:
Meneja
Kituo Kikuu cha Utabiri TMA, Bw. Samwel Mbuya akizungumza kwenye
mkutano na waandishi wa Habari (Hawapo pichani) wakati wa tukio hilo.
Kulia ni Afisa Uhusiano wa TMA, Bi. Monica Mutoni
Mkutano huo kwa waandishi wa Habari ukiendelea
Meneja
Kituo Kikuu cha Utabiri TMA, Bw. Samwel Mbuya ( katikati) akitoa
ufafanuzi wa taarifa hiyo kulia ni Afisa Uhusiano wa TMA, Bi. Monica
Mutoni na kushoto ni Afisa Habari wa Idara Habari MAELEZO, Bw. Frank
Mvungi.
Afisa
Uhusiano wa TMA, Bi. Monica Mutoni (kulia) akizungumza katika mkutano
huo. Katikati ni Meneja Kituo Kikuu cha Utabiri TMA, Bw. Samwel Mbuya
na kushoto ni Afisa Habari wa Idara Habari MAELEZO, Bw. Frank Mvungi.
(Picha zote na Andrew Chale,
0 maoni:
Chapisha Maoni