Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbawara, ameagiza
kituo cha kuhifadhi kumbukumbu (Data centre) mbalimbali cha Kijitonyama
jijini Dar-es-salaam kianze kufanya kazi mara moja, kwa madai kituo
hicho muhimu kikiendelea bila kufanya kazi, kinaitia hasara kubwa
serikali.
Waziri huyo ametoa agizo hilo wakati akikagua njia ya mkongo wa taifa eno la kijiji cha Iguguno wilaya ya Mkalama, Singida.
Alisema
kituo hicho kwa sasa kinaendelea kuitia hasara serikali kwa kuingia
gharama mbalimbali ikiwemo ya umeme na mishahara ya wafanyakazi kutokana
na kutokuanza kazi, wakati kimekamilika kujengwa muda mrefu.
“Sielewi
kuna sababu gani inakwamisha kituo hicho kuanza kazi wakati wateja wake
wako wengi, na wanasubiri tu kituo kianze kufanya kazi. Pengine ni
watumishi wake wanafanya kazi kwa mazoea … TTCL wanasuasua na katibu
wangu mkuu, naye hasimamii kikamilifu kituo hichi ambacho ni kitega
uchumi kikubwa cha serikali,” alisema.
Waziri
Mbawara, alitumia fursa hiyo kumwagiza katibu wake mkuu upande wa
mawasiliano,ahakikishe anasimamia kikamilifu mradi huo ili uanze mapema
iwezekanavyo.
Waziri
wa ujenzi,uchukuzi na mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza
kushoto) akipewa maelezo juu ya mitambo ya simu ya TTCL mjini Singida
“Mradi
huu serikali imeukopea fedha nyingi na zinatakiwa kurejeshwa kwa
wakati. Sasa badala ya kituo kuanza kazi mapema, kimeendelea
kubaki bila kufanya kazi huku mambo yote muhimu,yameisha kamilika.
Hatuwezi kuruhusu hali hii ya kuitia hasara serikali, iendelee,”
alifafanua zaidi.
Kituo
hicho ambacho karibu kila nchi duniani inacho, kinatarajiwa kuweka au
kuhifadhi taarifa/kumbukumbu mbalimbali muhimu za taasisi za fedha,
makampuni na wadau ili endapo taasisi itapoteza taarifa zake muhimu
ikiwemo majengo kuugua moto,waweze kuzipata kwenye kituo hicho.
Katika
hatua nyingine, Meneja wa TTCL kanda ya kati, Peter Lusama, alisema
kampuni ya simu Tanzania (TTCL) mkoa wa Singida, imekusanya mapato yake
zaidi ya shilingi 132 milioni sawa na asilimia 180 ya lengo kati ya
Januari hadi Mei mwaka huu.
Alisema
mafanikio hayo yametokana na malipo mbalimbali kutoka kwa wateja 4,452
(1,490 wa simu za mezani, 2,932 wa simu za mkononi na wateja 30
walioungwa kupitia mkongo wa Taifa).
“Tukiangalia
mwenendo wa mahitaji ya huduma katika mkongo wa Satellite (Broad band)
hasa mradi wa simu za mkononi unaotarajiwa kuwa tayari mwezi huu wa
Juni, tuna uhakika wa kuyapandisha mapato na kuweza kufikia lengo la
mwaka huu, la zaidi ya shilingi 232.5 milioni,” alisema.
Hata
hivyo, meneja Lusama alisema pamoja na mafanikio hayo, wamekabiliwa na
changamoto ya deni kubwa la zaidi ya shilingi 94.8 Milioni na taasisi
za Serikali wameweka mikakati ya kuhakikisha deni hilo linalipwa mapema
iwezekanavyo.
Aidha,
meneja huyo alisema kama ilivyo kwa mikoa mingine, mkoa wa Singida nao
unapata mawasiliano kupitia katika mkongo wa Taifa wenye urefu wa
takribani Kilometa 433.
“Kati
ya Kilometa hizo 433, Kilometa 153 zimechimbiwa chini ya ardhi na
Kilometa 280 zinapita juu ya nguzo za TANESCO. Tunaendelea kutoa elimu
kwa wadau wote vijijini vinavyopitiwa na mkongo wa Taifa, ili waendelea
kuhakikisha usalama wa mkongo, unadumishwa,” alisema meneja huyo.
Lusama alisema
hata hivyo, hakuna matukio ya kuhujumu mkongo huo hadi sasa zaidi ya
maeneo korofi katika njia ya chini ambayo tumeshayatafutia ufumbuzi wa
kudumu.
Kwa
mujibu wa Meneja huyo, TTCL Mkoa wa Singida, inahudumia Wilaya tatu
kati ya tano zilizopo. Wilaya hizo ni Singida, Manyoni na Iramba, utoaji
wa huduma katika wilaya mpya za Ikungi na Mkalama, ziko katika hatua za
awali za ujenzi wa minara.
Na Nathaniel Limu
0 maoni:
Chapisha Maoni