Kaimu
Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Makwaia Makani
akimkaribisha Balozi wa China nchini Tanzania, Dk. LU Youqing ambaye
amefika kwenye hospitali hiyo LEO kwa ajili ya kuchangia damu katika
maadhimisho ya siku ya damu duniani.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Makani akisoma taarifa fupi kwa Balozi Dk. LU Youqing kabla ya kuchangia damu LEO.
Baadhi
ya madaktari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na wa China
wakimsikiliza Kaimu Mkurugenzi, Makani wakati akisoma taarifa fupi kwa
balozi huyo.
Balozi
wa China, Dk. LU Youqing nchini Tanzania akizungumza na waandishi wa
habari LEO katika hospitali hiyo. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi
ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa Mohammed Janabi na kulia ni
Kaimu Mkurugenzi wa MNH, Makwaia Makani.
Mkurugenzi
wa Upasuaji, John Kimaro na Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi, Praxeda
Ogweyo wakifuatilia mkutano huo Leo kwenye hospitali hiyo.
Kaimu
Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa
Mohammed Janabi akizungumza na waandishi wa habari kwenye hospitali
hiyo. Kutoka kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa MNH, Makani na Balozi wa
China, Dk. LU Youqing.
Sista Elizabeth Mweta akimwezesha Balozi wa China, Dk. LU Youqing kuchangia damu leo kwenye hospitali hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo akimkabidhi cheti Balozi Dk. LU Youqing baada ya kuchangia damu LEO.
Balozi Dk. LU Youqing akinywa chai baada ya kukamilisha shughuli ya uchangiaji damu leo katika hospili hiyo.
Picha na JOHN STEPHEN, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
……………………………………………………………………………………………….
Na Neeema Mwangomo, Dar es salaam
Balozi wa China nchini Dk. LU
Youqing leo amejitokeza kuchangia damu katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili (MNH) kwa lengo la kuwahamasisha wananchi kuwa na moyo wa
kuchangia damu, lakini pia kuadhimisha siku ya wachangia damu Duniani
ambayo huadhimishwa Juni 14 kila mwaka.
Balozi Youqing amesema
wakati tukiadhimisha siku hii muhimu, tunatukumbushwa kujenga
utamaduni wa kuchangia damu kwa upendo ili kuokoa maisha ya wale wenye
uhitaji wa damu.
Pamoja na mambo mengine, Balozi
Youqing amesisitiza kwamba Serikali ya China itaendelea kushirikiana
na Tanzania katika shughuli mbalimbali ikiwamo kuisaidia sekta ya
afya .
Awali akizungumza kabla ya
shughuli kuchangia damu, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa
Muhimbili Makwaia Makani amemshukuru Balozi huyo wa China kwa kuwa
Balozi wa kwanza wa kigeni kujitokeza kuchangia damu kwenye hospitali
hiyo kwani hatua hiyo imeonyesha ni jinsi gani anaguswa katika kuokoa
maisha ya Watanzania.
“Timu ya wataalamu
mbalimbali wa afya kutoka China wamekua na ushirikiano mzuri na wa muda
mrefu na hospitali hiyo katika kusaidia huduma za afya na tumekuwa
tukifanya nao kazi tangu mwaka 1968,” amesema Kaimu Mkurugenzi Makani.
Akifafanua amesema kimsingi
mahitaji ya damu ni makubwa kwani Hospitali ya Taifa Muhimbili
inahitaji chupa za damu 100 hadi 150 kwa siku, lakini chupa
zinazopatikana ni 60 na kwamba upungufu ni asilimia 25.
Kwa upande wake Mkuu wa Idara
ya Maabara wa MNH Dk, Alex Magesa amesema pamoja na jitihada
zinazofanywa na Hospitali hiyo za kukusanya damu, lakini zoezi hilo
linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo uchache wa vitanda
vinavyotumika wakati wa kutoa damu, jokofu kubwa la kiibailojia kwa
ajili ya kuhifadhia damu na usafiri wa kwenda kukusanya damu nje ya
Hospitali.
Katika kuadhimisha siku ya
wachangia damu duniani Hospitali ya Taifa Muhimbili inatembelea maeneo
mbalimbali ya wazi ikiwamo vyuoni ili kukusanya damu.
Maadhimisho hayo ambayo kitaifa yanafanyika mkoani Dodoma yamebeba kauli mbiu ‘Damu inaunganisha kila mtu.’
0 maoni:
Chapisha Maoni