Jumanne, 5 Aprili 2016

ULAJI WA CHAKULA UZINGATIE KANUNI ZA AFYA KWA MAENDELEO YA JAMII NA TAIFA.

imagesNa Eleuteri Mangi- MAELEZO
…………………………………………
Ni rahisi sana kutamka neno afya, neno hili linajenga dhana ya hali ya ukamilifu kimwili, kiakili, kijamii na kutokuwepo kwa maradhi ambayo huleta hali ya kuwa huru na kutokuwa na hali ya kuumwa au udhaifu wa mwili.
Kuwa na afya tu haitoshi, mwanadamu anapaswa kuwa na afya bora ambayo huchukuliwa kama nguzo na raslimali muhimu katika kuchangia maendeleo ya mtu binafsi, familia na nchi hususan katika kuleta maisha bora na kupunguza umaskini.
Kwa mantiki hiyo, afya bora inalenga kuwa na ustawi endelevu kwa jamii, kwa kuzingatia mchango wa mtu binafsi kulingana na nafasi, uwezo na fursa zilizopo katika kuleta maisha bora.
Upatikanaji wa afya bora unahitaji uwezeshaji wa jamii yenyewe iwe na uwezo wa kushiriki, kuamua, kupanga na kutekeleza mikakati yao ya kuwaletea maendeleo katika ngazi mbalimbali.
Ili kuwa na afya bora ni vizuri kujiuliza maswali kadhaa ambayo ndiyo yatajenga msingi imara wa afya ya mtu binafsi au jamii.
Maswali hayo ni pamoja na Unakula nini? Unakula kiasi gani? Unakula aina gani ya vyakula? Una lala kwenye nini? Unalala masaa mangapi kwa siku? Unafanya mazoezi? Unakula mara ngapi kwa siku?Unakunywa nini? Unapata hewa safi unapokuwa kazini au nyumbani? Unapata muda wa kwenda hospitali mara kwa mara kupima afya yako?
Maswali haya ni ya msingi katika kujenga afya bora kwa kuzingatia elimu ya afya na uhamasishaji miongoni mwa jamii unapaswa kuwa njia muhimu katika utoaji wa huduma za afya.
Njia hiyo inatumia utaalamu wa mawasiliano kwa kutayarisha na kuwasilisha ujumbe mbalimbali kwa mtu binafsi, familia na jamii kwa lengo la kubadilisha mienendo na tabia zinazochangia kuwepo au kutokuwepo kwa maradhi katika jamii.
Hali hiyo ya afya bora inapokuwa tofauti maana nayo hubadilika, watu wengine husema “Ninaumwa, ninahoma, sijisikii vizuri, ni mgonjwa n.k”.
Misemo hiyo ambayo hutumiwa kila mara huonesha mtu au jamii fulani afya yao sio nzuri, mara nyingi watu hawa na wale anaojiona ni wazima wanasahau wapo miongoni mwao wenye uzito mkubwa kupita kiasi ambapo hali hiyo inawafanya waonekane wanene kupita kiasi ambao huo ni ugonjwa.
Unene wa kupindukia hupelekea mwili kuwa na mafuta ya ziada ambayo hulimbikizana hadi kiwango kinachoweza kuathiri afya na kupelekea kupungua kwa matarajio ya mtu kuishi muda mrefu au kuwa na ongezeko kubwa la matatizo ya kiafya.
Utafiti mpya umeonesha watu wazima wengi duniani ni wanene kupita kiasi na kwamba hakuna matumaini ya kufikia lengo la kupunguza idadi ya watu wanene duniani.
Wanasayansi waliofanya utafiti huo ambao walitoka Chuo cha Imperial cha London, waliandika katika jarida la kimatibabu la Lancet la Uingereza, wanasema miongo minne iliyopita, kuwa na uzani wa chini kupita kiasi lilikuwa tatizo kubwa kuliko unene.

0 maoni:

Chapisha Maoni