Kama mnavyofahamu, Serikali
kupitia Wizara yangu imeweka utaratibu wa kutoa kila wiki taarifa ya
mwenendo wa mlipuko wa ugonjwa wa Kipindupindu nchini ili kuifahamisha
jamii hali ilivyo na hatua zinazochukuliwa na Wizara kudhibiti ugonjwa
huu. Hadi kufikia tarehe 17 April 2016, jumla ya wagonjwa 20,882
wametolewa taarifa, na kati ya hao ndugu zetu 329 wamepoteza maisha
tangu ugonjwa huu uliporipotiwa Agosti 2015.
Takwimu za wiki iliyopita kuanzia
tarehe 10 hadi 17 Aprili 2016 zinaonyesha kuwa, kasi ya ugonjwa wa
kipindupindu imepungua ambapo idadi ya wagonjwa wapya walioripotiwa wiki
hiyo ni 212 ikilinganishwa na 368 wa wiki iliyotangulia. (April 04
hadi Aprili 10, 2016). Mikoa ambayo bado imeendelea kuripoti ugonjwa wa
kipindupindu ni 10. Mikoa iliyopata wagonjwa wengi zaidi ni Morogoro
(wagonjwa 51 na Kifo 1), Mara (45), Kilimanjaro (31), Pwani (24), na
Tanga (24). Aidha hakuna Mkoa mpya uliotoa taarifa ya kuwepo kwa
wagonjwa wa Kipindupindu.
Pia katika wiki hii Halmashauri
zilizoongoza kuwa na wagonjwa wengi ni Morogoro vijijini (23), Same
(20), Tarime mjini (20), Mvomero (wagonjwa 18, na Kifo 1) na Kinondoni
(16). Vile vile, katika wiki hii Mikoa ambayo haijapata mgonjwa wa
Kipindupindu ni Kigoma, Dodoma, Singida, Shinyanga, Tabora, Lindi,
Kagera, Rukwa, Katavi, Mbeya, Simiyu, Iringa na Mtwara.
Tafsiri kubwa tunayoipata kutoka
kwenye takwimu hizi ni kwamba kwa sasa ni dhahiri kuwa juhudi zetu za
pamoja za kupambana na ugonjwa wa Kipindupindu zimeonyesha matunda.
Wizara inawapongeza wadau wote kwa jitihada za dhati zinazoendelea
kutekelezwa na katika kusimamia kikamilifu miongozo inayotolewa na
Wizara .
Vile vile, napenda kusisitiza
kwamba pamoja na kwamba tuna Mikoa ambayo haijaripoti wagonjwa au mikoa
ambayo imekuwa haina wagonjwa wapya kwa muda, bado hali si salama,
hususani wakati huu wa mvua za masika, na kwa kuwa na uwepo wa
mwingiliano mkubwa wa watu kwa ajili ya shughuli mbalimbali za usafiri
na za biashara. Hali hii bado inaweza kupelekea ugonjwa wa Kipindupindu
kuenezwa kutoka mkoa wenye uambukizo na kwenda kwenye mikoa mingine.
Hivyo ni budi mikoa yote nchini kuendelea kuchukua hatua za tahadhari
ili kuzuia maambukizi, na pia kuendelea kutoa taarifa za ugonjwa kila
siku, hata kama hakuna wagonjwa, na kusimamia kikamilifu hatua
mbalimbali za udhibiti wa mlipuko huo.
0 maoni:
Chapisha Maoni