Jumanne, 19 Aprili 2016

TAMKO KUHUSU MWENENDO WA UGONJWA WA KIPINDUPINDU NCHINI LILILOTOLEWA NA MHE. UMMY MWALIMU WAZIRI WA AFYA LEO

um1
Kama mnavyofahamu, Serikali kupitia Wizara yangu imeweka utaratibu wa kutoa kila wiki taarifa ya mwenendo wa mlipuko wa ugonjwa wa Kipindupindu nchini  ili kuifahamisha jamii hali ilivyo na hatua zinazochukuliwa na Wizara  kudhibiti ugonjwa huu. Hadi kufikia tarehe 17 April 2016, jumla ya wagonjwa 20,882 wametolewa taarifa, na kati ya hao ndugu zetu 329 wamepoteza maisha tangu ugonjwa huu uliporipotiwa Agosti 2015.
Takwimu za wiki iliyopita kuanzia tarehe 10 hadi 17 Aprili 2016 zinaonyesha kuwa, kasi ya ugonjwa wa kipindupindu imepungua ambapo idadi ya wagonjwa wapya walioripotiwa wiki hiyo ni 212  ikilinganishwa na 368 wa wiki iliyotangulia.  (April 04 hadi  Aprili 10, 2016). Mikoa ambayo bado imeendelea kuripoti ugonjwa wa kipindupindu ni 10. Mikoa iliyopata wagonjwa wengi zaidi ni Morogoro (wagonjwa 51 na Kifo 1), Mara (45), Kilimanjaro (31), Pwani (24), na Tanga (24). Aidha hakuna Mkoa mpya uliotoa taarifa ya kuwepo kwa wagonjwa wa Kipindupindu.
Pia katika wiki hii Halmashauri zilizoongoza kuwa na wagonjwa wengi ni Morogoro vijijini (23), Same (20), Tarime mjini (20), Mvomero (wagonjwa 18, na Kifo 1) na Kinondoni (16). Vile vile, katika wiki hii Mikoa ambayo haijapata mgonjwa wa Kipindupindu ni Kigoma, Dodoma, Singida, Shinyanga, Tabora, Lindi, Kagera, Rukwa, Katavi, Mbeya, Simiyu, Iringa na Mtwara.
Tafsiri kubwa tunayoipata kutoka kwenye takwimu hizi ni kwamba kwa sasa ni dhahiri kuwa juhudi zetu za pamoja za kupambana na ugonjwa wa Kipindupindu zimeonyesha matunda. Wizara inawapongeza wadau wote kwa jitihada za dhati zinazoendelea kutekelezwa na katika kusimamia kikamilifu  miongozo inayotolewa na Wizara .
Vile vile, napenda kusisitiza kwamba pamoja na kwamba tuna Mikoa ambayo haijaripoti wagonjwa au mikoa ambayo imekuwa haina wagonjwa wapya kwa muda, bado hali si salama, hususani wakati huu wa mvua za masika, na kwa kuwa na uwepo wa mwingiliano mkubwa wa watu kwa ajili ya shughuli mbalimbali za usafiri na za biashara. Hali hii bado inaweza kupelekea ugonjwa wa Kipindupindu kuenezwa kutoka mkoa wenye uambukizo na kwenda kwenye mikoa mingine. Hivyo ni budi mikoa yote nchini kuendelea  kuchukua hatua za tahadhari ili kuzuia maambukizi, na pia kuendelea kutoa taarifa za ugonjwa kila siku, hata kama hakuna wagonjwa, na kusimamia kikamilifu hatua mbalimbali za udhibiti wa mlipuko huo.

0 maoni:

Chapisha Maoni