Mtoto huanza kujifunza kulingana
na mazingira yake yanayomzunguka, mafunzo hayo yanamuwezesha kupata
uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile ili
aweze kuyamudu mazingira yake.
Hali hiyo inajenga dhana ya kupata elimu kulingana na mazingira ambayo hujulikana kama elimu isiyo rasmi.
Ni vema ikaeleweka kwamba
tunapozungumza kuhusu watoto, tunazikusudia jinsia zote mbili, yaani
watoto wa kike na wale wa kiume. Katika hali halisi ndani ya maisha ya
kijamii, elimu ni nyenzo ambayo hutumiwa kupitisha maarifa, ujuzi na
maadili kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine bila kujali jinsia.
Elimu kwa watoto wa kike ni moja ya njia bora za kupunguza umaskini katika mataifa yanayoendelea ikiwemo Tanzania.
Manufaa hayo ya elimu kwa watoto wa kike yanaweza kuonekana kwa mtu binafsi, familia zao, jamii yote na taifa kwa ujumla.
Ni dhahiri, manufaa
yanayopatikana kupita elimu ni mengi katika jamii ikiwemo kupunguza
idadi ya watoto ambao wanawake hujifungua, kupunguza idadi ya vifo vya
watoto wadogo, kupunguza idadi ya vifo vya akina mama, kuwalinda dhidi
ya maambukizo ya VVU/UKIMWI na kuongeza idadi ya wanawake wenye kazi na
mapato ya juu ambayo hudumu kwa vizazi vingi.
Hakika ukimuelimisha mtoto wa
kike, umemsaidia kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi bora kwa manufaa yake,
familia yake na hata taifa.
Hali hii imechukua sura mpya
nchini Tanzania ambapo Serikali, watu binafsi, mashirika ya dini na
taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi zimekuwa mstari wa mbele
kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu ambayo ndiyo kinga na urithi
pekee ambao hawezi kunyang’anywa wala kugawana na mtu mwingine ndani ya
familia na hata jamii inayomzunguka.
Sura hiyo mpya imeoneshwa na
Mfuko wa Graca Machel (Graca Machel Trust) ambao umejikita katika
kusaidia wanawake na watoto nchi kadhaa Barani Afrika.
Taasisi hiyo imebisha hodi na
kukaribishwa nchini Tanzania mkoa wa Mara ambapo imeazimia kuwasaidia
watoto wa kike 20,000 ndani ya mkoa huo ambao watanufaika kwa fursa ya
kupata elimu.
Mapema Aprili 6, 2016 Waziri wa
Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI),
Mhe. George Simbachawene alibainisha Mfuko wa Graca Machel umeamua
kuwasaidia watoto wa kike wa mkoa wa Mara mara baada ya kukutana na
kufanya mazungumzo na Mama Graca Machel alipomtembelea ofisini jijini
Dar es salaam.
0 maoni:
Chapisha Maoni