Jumanne, 19 Aprili 2016

Taasisi ya Graca Machel mdau muhimu wa elimu ya mtoto wa kike nchini, ikiwa na lengo la kuielimisha jamii.


GRANa Eleuteri Mangi-MAELEZO
Mtoto huanza kujifunza kulingana na mazingira yake yanayomzunguka, mafunzo hayo yanamuwezesha kupata uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile ili aweze kuyamudu mazingira yake.
Hali hiyo inajenga dhana ya kupata elimu kulingana na mazingira ambayo hujulikana kama elimu isiyo rasmi.
Ni vema ikaeleweka kwamba tunapozungumza kuhusu watoto, tunazikusudia jinsia zote mbili, yaani watoto wa kike na wale wa kiume. Katika hali halisi ndani ya maisha ya kijamii, elimu ni nyenzo ambayo hutumiwa kupitisha maarifa, ujuzi na maadili kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine bila kujali jinsia.
Elimu kwa watoto wa kike ni moja ya njia bora za kupunguza umaskini katika mataifa yanayoendelea ikiwemo Tanzania.
Manufaa hayo ya elimu kwa watoto wa kike yanaweza kuonekana kwa mtu binafsi, familia zao, jamii yote na taifa kwa ujumla.
Ni dhahiri, manufaa yanayopatikana kupita elimu ni mengi katika jamii ikiwemo kupunguza idadi ya watoto ambao wanawake hujifungua, kupunguza idadi ya vifo vya watoto wadogo, kupunguza idadi ya vifo vya akina mama, kuwalinda dhidi ya maambukizo ya VVU/UKIMWI na kuongeza idadi ya wanawake wenye kazi na mapato ya juu ambayo hudumu kwa vizazi vingi.
Hakika ukimuelimisha mtoto wa kike, umemsaidia kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi bora kwa manufaa yake, familia yake na hata taifa.
Hali hii imechukua sura mpya nchini Tanzania ambapo Serikali, watu binafsi, mashirika ya dini   na taasisi mbalimbali za ndani na nje ya nchi zimekuwa mstari wa mbele kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu ambayo ndiyo kinga na urithi pekee ambao hawezi kunyang’anywa wala kugawana na mtu mwingine ndani ya familia na hata jamii inayomzunguka.
Sura hiyo mpya imeoneshwa na Mfuko wa Graca Machel (Graca Machel Trust) ambao umejikita katika kusaidia wanawake na watoto nchi kadhaa Barani Afrika.
Taasisi hiyo imebisha hodi na kukaribishwa nchini Tanzania mkoa wa Mara ambapo imeazimia kuwasaidia watoto wa kike 20,000 ndani ya mkoa huo ambao watanufaika kwa fursa ya kupata elimu.
Mapema Aprili 6, 2016 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. George Simbachawene alibainisha Mfuko wa Graca Machel umeamua kuwasaidia watoto wa kike wa mkoa wa Mara mara baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Mama Graca Machel alipomtembelea ofisini jijini Dar es salaam.

0 maoni:

Chapisha Maoni