Ijumaa, 8 Aprili 2016

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein awaongoza wazanzibari kumbukumbu ya Karume


kare
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein leo amewaongoza viongozi na wananchi mbali mbali katika kisomo maalum cha kumuombea dua Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi marehemu Sheikh Abeid Amani Karume ikiwa pia, ni maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 44 ya kifo chake.
Marehemu Mzee Karume ambaye pia, alikuwa Kiongozi wa Chama cha Afro-Shirazi (ASP) na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliuawa siku ya Ijumaa tarehe 07 April, 1972 saa 12:05 jioni katika Makao Makuu ya ASP ambayo sasa ni Ofisi Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) iliyopo Kisiwandui mjini Unguja.
Katika maadhimisho hayo yaliyofanyika Ofisi Kuu ya CCM ambako ndipo alipozikwa marehemu, Dk. Shein na viongozi mbalimbali pamoja na wananchi walishiriki kisomo maalum cha kumuombea dua kiongozi huyo ambaye kifo chake kiliushitua ulimwengu mzima.
Baada ya kisomo hicho viongozi hao walizuru kaburi la marehemu wakiambatana na viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini ambao walipewa fursa za kumuombea dua marehemu wakiwa kaburini hapo.
Kisomo hicho cha kumuombea dua Marehemu Mzee Karume kilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na Rais mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Sita, Mhe. Amani Abeid Karume.
Viongozi wengine walihudhuria katika hitma hiyo ni  Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mzee Ali Hassan Mwinyi, Spika wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Zubeir Ali Maulid, Mufti Mkuu wa Tanzania Bara Sheikh  Abubakar Zubeir, Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji, Sheikh wa Mkoa wa Dar-es- Salam Sheikh Mussa Salum.

0 maoni:

Chapisha Maoni