Jumanne, 19 Aprili 2016

Madiwani Wete Kisiwani Pemba wala kiapo kupambana na wakwepa kodi

8022
Na Masanja Mabula –Pemba
MADIWANI wa wadi kumi zinazounda Baraza la Mji Wete Kisiwani Pemba  , wamekula kiapo cha utii na kuahidi kushirikiana na Uongozi wa Baraza hilo katika kupambana na wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi .
Wakizungunza na mwananchi baada ya kiapo hicho kilichosimamiwa na Hakimu wa Mahakama ya Mkoa wa Kaskazini Pemba ,  Isihaka Ali Khamis , waliapa kuziba mianya yote inayotumiwa na wafanyabiashara kuikosesha mapato Serikali .
Walisema kwamba katika utendaji wao wa kazi hawatamuonea mtu kwa sababu  za kisiasa , bali watahakikisha kila anayehusika na ulipaji  kodi anatimiza wajibu wake kisheria.
Ali Shariff Omar Diwani wa Wadi ya Bopwe alisema , anafahamu mbinu zinazotumiwa na baadhi ya wafanyabiashara kuingia bidhaa kienyeji na kuwataka wafanyabiashara hao kujisalimisha kwani hawatakuwa tena na fursa hiyo .
“Nawaomba wafanyabiashara watubu na wajisalmishe mapema , kwani mbinu na mianya wanayoitumia kukwepa kodi zinajulikana  , kwa hili hakuna huruma na hataonewa mtu kwa misingi ya kisiasa ”alieleza .
Kwa upande wake Diwani wa wadi ya Piki Asha Khamis Nassor alisema mbali na kudhibiti mianya ya wakwepa kodi , pia aliahidi kuimarisha vikundi vya ushirika ambavyo vimekuwa vikizalisha ajira kwa vijana hususani wanawake .
Alisema katika kuviimarisha vikundi hivyo , hakutakuwa na ubaguzi wa vyama vya siasa huku akiwaomba wanawake wenzake kuumuunga mkono ili aweze kufanikisha malengo aliyoyakusudia .
“Nimekuja na muono wa mbali wa kuviimarisha vikundi vya ushirika katika wadi yangu , hii itasaidia kuongeza ajira kwa vijana hususani wanawake , kwa hili naomba ushirikiano wao ”alisema .
 Mapema katika nasaha zake kwa Madiwani Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Om,ar Khamis Othman aliwataka kutekeleza majukumu yao ya kazi kwa kuwatumikia wananchi wote bila ya kuwabagua kwa misingi ya vyama vyao  hasa kwa kuzingatia  sheria  za tawala za mikoa namba 4 /2014.
Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala Mkoa huo  Yussuf Mohammed Ali aliwasisitiza madiwani hao kutobweteka na ushindi pamoja na dhamana  zao mpya , bali wajipange kusimamia kazi kwa kushirikiana nawatendaji wa  baraza la mji .
 
“Wacheni kubweteka na ushindi ulioupata pamoja na dhamana zenu hizi mpya , bali jipangeni kusimamia majukumu yenu kwa kushirikiana na watendaji wa Baraza la Mji ”alifahamisha Tawala .
Mapema Mkurugenzi wa Baraza la Mji Wete Mgeni Othman Juma aliwataka madiwani hao kuwa waadilifu katika kusimamia mapato ya baraza ili fedha zinazokusanywa ziweze kutumika katika miradi ya maendeleo ya wananchi .
 
Madiwani hao kutoka chama Cha Mapinduzi (CCM ) walichaguliwa kushika nafasi hizo katika uchaguzi Mkuu uliofanyika machi 20 mwaka huu , uchaguzi ambao ulisusiwa na Chama  Cha Wananchi (CUF) ambacho ndiyo chama kikuu cha Upinzani Zanzibar .
 

0 maoni:

Chapisha Maoni