Alhamisi, 26 Januari 2017

JAJI MKUU WA ZANZIBAR AWATAKA MAHAKIMU KUZINGATIA MAADILI YA KAZI ZAO

Posted by Esta Malibiche on JAN 27,2017 IN NEWS

MAKUNGU
Khadija Khamis –Maelezo
Jaji  Mkuu wa Zanzibar  Omar Othman Makungu  amewataka  Mahakimu, makadhi na  wasuluhishaji  wa migogoro ya kazi kutekeleza majukumnu yao kwa  uwadilifu wakizingatia kutoa haki kwa wanaostahiki kupata haki hizo.
Jaji Makungu  aliyasema hayo katika hafla ya kuwaapisha Makadhi wa Wilaya, Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo na wasuluhishi na waamuzi wa migogoro ya kazi chini ya kamisheni ya kazi  katika mahakama kuu  Vuga.
Aliwaeleza wasimamizi hao wapya wa sheria  kuwa  majukumu waliyokabidhiwa na Taifa sio mepesi na kuwataka kuzingatia maadili ya kazi ili haki na sheria iweze kuchukua nafasi yake.
Aidha alisema usuluhishi na utoaji maamuzi panapotokea migogoro katika sehemu za  kazi inasaidia  katika kujenga umoja na ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi.
Waliapishwa kuwa Makadhi wa Mahakama ya Wilaya ni  Idi Said Khamis na Sleiman Khamis Machano,  Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo ni Hakimu  Amina Mohd Makame na Hamad Ali Sleiman, wasuluhishaji na waamuzi wa migogoro ya kazi ni Fatma  Abdalla Hamad, Jokha Lali Ramadhani , Juma Ali Makame na Raya Said Ali .
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya siku ya sheria duniani ambayo kilele chake ni tarehe tisa ya kila mwaka, Jaji Mkuu Omar Othman Makungu alisema shamra shamra za sherehe hiyo zitaanza tarehe nne mwezi ujao kwa matembezi ya hiari.
Aliongeza kuwa katika maadhimisho hayo kutakuwa na maonyesho ya sheria, utoaji wa vyeti  kwa mawakili wapya na uzinduzi wa mahakama ya watoto katika kijiji cha Mahonda Wilaya ya Kaskazi B.
Alifahamisha kuwa  kutakuwa na mikakati ya mipango kazi ambayo itasaidia kufanya kazi kwa wakati muafaka na kuwepo na utaratibu maalumu wa kuamua kesi ili kuepuka msongamano wa kesi katika mahakama ili kupunguza malalamiko kutoka kwa wananchi.
Jaji Mkuu wa Zanzibar alisema kaulimbiu ya siku ya sheria duniani mwaka huu ni kusimamia sheria na maadili katika kutenda haki.

0 maoni:

Chapisha Maoni