Ijumaa, 13 Januari 2017

WAKULIMA WA KOROSHO WILAYA YA KILWA MKOANI LINDI KUPEWA BURE MICHE YA MIKOROSHO

Posted by Esta Malibiche on JAN 13,2017 in NEWS

Miche ya Mikorosho


Lindi Yetu


Na. Ahmad Mmow, Lindi.
Katika harakati za kuongeza uzalishaji wa zao la korosho wilayani Kilwa mkoani Lindi, halmashauri ya wilaya hiyo kupitia idara yake ya kilimo inatarajia kugawa bure miche 50000 ya zao hilo kwa wakulima katika msimu huu wa kilimo wa 2017/2018.
Akizungumza kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, mwanzoni mwa wiki hii katika kijiji cha Lihimalyao Kusini, mkuu wa idara ya kilimo ya halmashauri hiyo, John Mkinga, alisema halmashauri ya wilaya ya Kilwa inamkakati kabambe wa kuongeza kiwango cha uzakishaji wa mazao ya biashara na chakula katika wilaya hiyo.

Ambapo kwa msimu huu idara hiyo inatarajia kugawa kwa wakulima miche 50000 ya mikorosho. Mkinga ambae alieleza hayo kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Zabron Bugingo, baada ya kutakiwa na mkuu wa mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi kujibu malalamiko ya wananchi ambao hadi sasa hawatambuliki ambao walipeleka barua kwa waziri wa TAMISEMI na Rais zenye malalako. Ikiwamo wilaya hiyo kutelekezwa katika sekta ya kilimo.

Alisema huo utakuwa ni mwendelezo wa juhudi za kuhakikisha kiwango cha uzalishaji wa zao hilo Katika wilaya hiyo unaongezeka ili kuongeza kipato cha wakulima, halmashauri na taifa kwa jumla.
"Msimu wa mwaka jana tulizalisha na kugawa bure miche 12000 kwa wakulima. Ikiwamo wakulima wa kata hii na tarafa ya Pande, pia tuligawa mbegu kwa baadhi ya wakulima na mpango huo ni endelevu," alisema Mkinga.

Kuhusu uzalishaji wa mazao ya chakula, Mkinga alisema serikali inatambua umuhimu na faida ya nchi kujitosheleza kwa chakula. Kwakutambua hilo, idara ya kilimo ya halmashauri hiyo imekuwa ikipeleka maombi serikali kuu ya kupatiwa matrekta kwa ajili ya kuyagawa kwa wakulima ili kuongeza uzalishaji wa mazao hayo wilayani humo.

Mkuu huyo wa idara ya kilimo alibainisha kwamba hadi sasa baadhi ya vijiji wilayani humo, ikiwamo baadhi ya vijiji vilivyopo katika tarafa ya Pande vimepatiwa matrekta.
"Napenda kuwashauri wakulima waunde vikundi kwasababu matrekta hayo hatumpi mkulima mmojammoja, mwaka huu tumeomba tena na tukipewa tutagawa katika vijiji vingine," alisema Mkinga. 

Aidha aliwahakikishia wakulima wa korosho kwamba dawa za kuuwa wadudu na kuzuia ukungu zitafikishwa kwao kabla ya mwezi Aprili mwaka huu, ili waweze kuzitumia kwa wakati.

Mkuu wa mkoa Zambi alikwenda kijijini hapo ikiwa ni utekelezaji wa agizo la waziri wa nchi ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene. Aliyemtaka kwenda wilayani humo, hususani tarafa ya Pande na kata ya Lihimalyao. Ili kupata ukweli wa barua zilizotumwa na watu ambao hadi sasa hawajafahamika kwenda kwake yeye na Rais Magufuli.

Ingawa walitumia majina na kughushi saini za baadhi ya viongozi wa vijiji vya Lihimalyao Kusini, Rushungi na kata ya Lihimalyao. Barua zilikuwa na malalamiko mbalimbali dhidi ya serikali kwamba wilaya hiyo imetupwa katika huduma za jamii, hakuna usalama, maliasili na rasimali zinaporwa na haziwanufaishi, wilyaa hiyo inawalimu wa shule za msingi wasio na sifa hakuna maji na hakuna juhudi zozote zilizofanywa na serikali katika kuondoa tatizo la maji na matumizi ya jembe la mkono katika tarafa ya Pande na wilaya kwa jumla. 

Hata hivyo malalamiko mengi yalionekana ni ya uongo. Huku viongozi wa vijiji hivyo na kata hiyo ambao majina yao yametumika kwenye barua hizo walikanusha kuandika na kumuomba mkuu huyo wa mkoa kupitia vyombo vya ulinzi na usalama awatafute, awakamate na awafikishe kwenye vyombo vya sheria walioandika barua hizo. 

Kwa madai kwamba yaliyoekelezwa kwenye barua hizo yalikuwa ya uongo na dalili ya uchochezi baina ya wananchi na serikali yao.

0 maoni:

Chapisha Maoni