Jumatano, 18 Januari 2017

MKUU WA MKOA WA IRINGA AMINA MASENZA AWACHARUKIA WATENDAJI WA SERIKALI WANAOSHINDWA KUTEKELEZA MAAGIZO YANAYOTOLEWA.

Posted by Esta Malibiche on JAN 18,2017 IN NEWS

MKUU wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza amecharuka na kutoa onyo kali kwa watendaji wa serikali wanaoshindwa au kupuuza utekelezaji wa maagizo yanayotolewa kwao kwa njia mbalimbali yakiwemo mafunzo.
“Sitaki longolongo ziendelee, taarifa zenu za utendaji mnazoandika mkiwa mmekaa kwenye madawati yetu ofisini ni marufuku. Asiyetaka kutekeleza majukumu ya serikali kwa vitendo aseme ili tumuondoe,” Masenza alisema.
Aliyasema hayo juzi mjini Iringa kwenye kikao maalumu cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kilichopokea na kupitia taarifa ya hali ya upatikanaji na utumiaji wa huduma za kifedha mkoani Iringa.
Taarifa hiyo iliwasilishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Kuendeleza Hudumza ya Fedha Tanzania (FSDT), Sosthenes Kewe.
Masenza alisema taarifa za utafiti wa kutambua na kupima mahitaji na upatikanaji wa huduma za fedha miongoni mwa wananchi zina umuhimu mkubwa kwa maendeleo yahusuyo upatikanaji wa huduma jumuishi za fedha.
“Kwahiyo watendaji wa serikali wa ngazi zote mnatakiwa kuzitumia taarifa za tafiti hizo kuboresha upatikanaji na utumiaji wa huduma za fedha katika maeneo yenu,” alisema.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa FSDT, Kewe alisema; “tumekutana na wajumbe wa RCC wa mkoa wa Iringa tukilenga kutoa taarifa ya upatikanaji na utumiaji wa huduma za fedha katika mkoa na kupima kama wanatakwimu za kutosha zinazosaidia kufanya maamuzi mbalimbali ya kisera.”
Alisema utafiti wa mwaka 2013 uliofanywa na taasisi ya FinScope, unaonesha Iringa ni mkoa wa pili nchini baada ya Dar es Salaam kwa kutumia huduma za kibenki na wa tano kwa kutumia huduma za fedha.
Alisema hali halisi ya upatikanaji na utumiaji wa huduma hizo unazingatia upatikanaji wa fursa nyingi za kiuchumi kikiwemo kilimo na ufugaji.
Ili kuboresha taarifa za upatikanaji na utumiaji wa hudumia hizo, Kewe alisema FinScope itafanya utafiti mwingine mwaka huu ili matokeo yake yatumike kupanga mipango ya kuboresha maeneo mbalimbali ya kisera katika ngazi ya serikali za mitaa.
“Tumechagua mikoa mitatu ya Iringa, Rukwa na Mwanza ambayo uchambuzi wa utafiti huo utakaofanywa mapema mwaka huu utatoa picha halisi ya upatikanaji wa huduma hizo kiwilaya na mikoa mingine inayobaki uchambuzi wake utakuwa wa ngazi ya mkoa,” alisema.
Alisema wamechagua Iringa kwasababu ya fursa kubwa ya kilimo waliyonayo, Rukwa kwasababu hauna huduma za kutosha za kifedha na Mwanza watakakofuatilia kwa kina shughuli za ujasiriamali.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alishukuru mkoa wa Iringa kuingizwa katika mikoa mitatu ambayo uchambuzi wa utafiti huo utafanywa hadi kwa ngazi ya wilaya.

“Takwimu zikichanganuliwa kiwilaya, itatusaidia kujipanga na kujiwekea mikakati ya makusudi katika maeneo yote yatakayoonekana yana mahitaji zaidi ya huduma hizo,” alisema.

0 maoni:

Chapisha Maoni