Postedy by a Esta Malibiche on August 12.2016 in News with No comment
Waziri wa Nishati na Madini,
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akisalimiana na sehemu ya watendaji
kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) pamoja na wakandarasi
wanaosimamia miradi ya umeme vijijini inayosimamiwa na Wakala wa
Nishati Vijijini (REA) mara baada ya kuwasili wilayani Handeni mkoani
Tanga.
Meneja wa Shirika la Umeme
Tanzania (TANESCO) mkoani Tanga Mhandisi Abdulrahman Nyenye akisoma
taarifa ya utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini chini ya Wakala wa
Nishati Vijijini (REA) mbele ya Waziri wa Nishati na Madini Profesa
Sospeter Muhongo pamoja na watendaji wengine kutoka Ofisi ya Mkuu wa
Mkoa wa Tanga, Wilaya ya Handeni, Wizara ya Nishati na Madini, TANESCO
na wakandarasi wanaotekeleza miradi ya REA.
Waziri wa Nishati na Madini
Profesa Sospeter Muhongo (kulia) na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine
Shigela (kushoto) wakifuatilia taarifa ya utekelezaji wa miradi ya
umeme vijijini inayosimamiwa na REA Awamu ya Pili (REA II) iliyokuwa
inasomwa na Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani
Tanga Mhandisi Abdulrahman Nyenye (hayupo pichani)
Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine
Shigela akielezea mafanikio ya miradi ya usambazaji wa umeme vijijini
iliyotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini Awamu ya Pili (REA II)
………………………………………………………………………………….
Na Greyson Mwase, Tanga
Waziri wa Nishati na Madini
Profesa Sospeter Muhongo amesema kuwa serikali imeweka mikakati ya
kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2020 kila mwananchi anapata umeme wa
uhakika na kupelekea uchumi wa nchi kukua kwa kasi.
Profesa Muhongo aliyasema hayo
mara baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa miradi ya usambazaji wa
umeme vijijini inayosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini Awamu ya
Pili (REA II) kutoka kwa watendaji wa Shirika la Umeme Tanzania
(TANESCO) mkoani Tanga. Profesa Muhongo yupo mkoani Tanga kwa ajili ya
kukagua miradi ya umeme vijijini inayotekelezwa na REA pamoja na
kuzungumza na wananchi.
Profesa Muhongo alisema kuwa kwa
kutambua mchango wa nishati ya umeme katika ukuaji wa viwanda nchini,
serikali imeweka mkakati wa kuhakikisha kuwa kasi ya usambazaji wa
umeme vijijini inaongezeka ili ifikapo mwaka 2020 mgawo wa umeme uwe
ni historia
Alieleza kuwa serikali imeamua
kuweka nguvu katika usambazaji wa umeme hususan katika maeneo ya
vijijini ili kufuta umaskini kwani kupitia nishati ya umeme wananchi
waishio vijijini wana uwezo wa kuanzisha viwanda vidogo vidogo na
kuongeza ajira na kupunguza wimbi la vijana wengi kukimbilia mijini kwa
ajili ya kutafuta maisha.
Akielezea mpango wa utekelezaji wa
miradi ya umeme vijijini itakayosimamiwa na REA Awamu ya Tatu (REA
III), Profesa Muhongo alisema kuwa serikali imetenga zaidi ya shilingi
trilioni moja kwa ajili ya kusambaza umeme katika maeneo yote
kipaumbele kikiwa ni katika vijiji vilivyokosa umeme REA Awamu ya Pili.
(REA II)
Hata hivyo Profesa Muhongo
alieleza kuwa wakandarasi waliokwamisha miradi ya REA Awamu ya Pili
hawatapewa kazi ya kusambaza umeme vijijini katika REA Awamu ya Tatu.
“Serikali iko makini katika
kuhakikisha kuwa wakandarasi wenye sifa wanapewa kasi ya kusambaza umeme
vijijini, hatuhitaji wakandarasi wasiotekeleza miradi kwa wakati,”
alisema Profesa Muhongo.
Profesa Muhongo aliwataka
wakandarasi wa kitanzania wenye vigezo kujitokeza na kuchangamkia fursa
ya kusambaza umeme vijijini kupita REA Awamu ya Tatu.
Aliongeza kuwa kupitia REA Awamu
ya Pili wakandarasi wa kitanzania walionyesha uwezo mkubwa sana katika
kusambaza umeme vijijini.
Ili kuendana na mahitaji ya umeme
nchini Profesa Muhongo alilitaka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO)
kuhakikisha linaongeza Megawati 200 za ziada ndani ya miezi 18.
Alisema wakati serikali kupitia
REA ikiendela na kasi yake ya kusambaza umeme nchi nzima, shirika la
TANESCO linatakiwa kuhakikisha nishati ya uhakika inapatikana ikiwa ni
pamoja na ubunifu wa vyanzo vipya vya umeme.
Awali akielezea utekelezaji wa
miradi ya umeme vijijini mkoani Tanga, Meneja wa Shirika la Umeme
Tanzania mkoani Tanga, Mhandisi Abdulrahman Nyenye alisema kuwa miradi
ya umeme vijijini chini ya ufadhili wa REA imekuwa ikitekelezwa katika
wilaya zote nane za mkoa wa Tanga ambazo ni pamoja na Tanga Mjini,
Muheza, Korogwe, Handeni, Kilindi, Lushoto, Pangani na Mkinga ambazo
zinapata umeme wake kutoka Gridi ya Taifa kupitia vituo vya Hale, Kange
na Tanga (Majani Mapana)
Alisema kundi la kwanza
lilihusisha wilaya za Korogwe, Lushoto, Handeni na Kilindi ambapo
mradi wa wilaya hizi ulitekelezwa na mkandarasi STEG International
Services Ltd ya Tunisia na kusimamiwa na TANESCO.
Alifafanua kuwa gharama za mradi
huo ilikuwa ni Dola za Marekani 9,463,502 ambazo ni sawa na shilingi
bilioni 14.6 na kuendelea kusema kuwa kundi la pili lilihusisha wilaya
za Muheza, Mkinga, Tanga Vijijini na Pangani na kutekelezwa na
mkandarasi Sengerema Engineering Group Ltd ya Tanzania na kusimamiwa na
TANESCO.
Alisema kuwa mradi huu uligharimu
shilingi bilioni 15.6 na kusisitiza kuwa miradi yote kwa mkoa wa Tanga
imekamilika kwa asilimia 99 ambapo jumla ya vijiji 178 vimepatiwa
huduma ya umeme
Akielezea changamoto katika
utekelezaji wa miradi hiyo Mhandisi Nyenye alieleza kuwa ni pamoja na
tatizo la wananchi kuzuia upitishwaji wa laini za umeme kwenye maeneo
yao kwa kudai fidia ili kuruhusu mazao yao yakatwe na hali ya hewa ya
mvua isiyotabirika hasa maeneo ya wilaya za Muheza na Lushoto.
Alitaja chagamoto nyingine kuwa ni
pamoja na ubovu wa miundombinu hasa ya barabara kwenye maeneo mengi ,
hali duni ya kiuchumi ya wananchi inayopelekea wananchi kushindwa
kulipa gharama za kuunganishiwa umeme na gharama kubwa za ukaguzi wa
miundombinu ya ndani (wiring) zinazotozwa na wakandarasi ambazo zimekuwa
ni kikwazo kwa wananchi wanaohitaji huduma ya umeme.
0 maoni:
Chapisha Maoni