Jumapili, 28 Agosti 2016

DC IKUNGI AWASWEKA RUMANDE VIONGOZI WANNE WA KIJIJI CHA KAUGERI

Postedy by Esta Malibiche on August 28.2016 in Newsnjo



Mkuu wa wilaya Ikungi, Miraji Mtaturu, akikagua ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Kaugeri wilayani humo ambayo mkandarasi ametoweka bila kukamilisha ujenzi.
…………………………………………………………………..
MKUU wa wilaya ya Ikungi mkoani Singida, Miraji Mtaturu, ameamuru kuwekwa ndani kwa viongozi wanne wa kijiji cha Kaugeri kilichopo katika wilaya hiyo kwa kosa la kuuza ardhi bila ya kufuata kanuni na taratibu zilizopo.
Aidha ameagiza kutafutwa  mkandarasi Samweli John na kuwekwa rumande  kutokana na kutokamilisha ujenzi wa Zahanati ya kijiji hicho wakati alishalipwa shilingi milioni 19.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara kijijini hapo, Mtaturu amesema watendaji hao wamegawa ardhi kwa mwekezaji zaidi ya hekta 150 na kuingia mikataba ya kiunyonyaji wakati kisheria kijiji hakitakiwi kutoa ardhi zaidi ya hekta 50 hivyo wamewekwa ndani mpaka jumatatu ili wahojiwe na kutoa maelezo na hatimaye maamuzi yafuate.
Amewataja waliosekwa rumande kuwa ni mwenyekiti wa kijiji cha Kaugeri Mange Nkuba, ,aliyekuwa kaimu mtendaji wa kijiji, Laurent Komba, na wajumbe wawili wa serikali ya kijiji, Paul Kilo na Aman Clement ambaye  anaendelea kutafutwa baada ya kutoroka kabla ya mkutano kufanyika.
Kuhusu ujenzi wa Zahanati hiyo ya Kijiji hicho, Mtaturu amesema mkandarasi huyo alitoweka toka mwaka 2013 na hivyo kufanya ujenzi huo kusimama wakati fedha alishachukua.
Kadhalika, ametoa muda wa mwezi mmoja kwa wananchi walio katika eneo la msitu uliotangazwa kuwa hifadhi toka mwaka 2003 kuondoka wenyewe katika eneo hilo kabla hawajatolewa kwa nguvu  kutokana na kuharibu mazingira.
Amewaasa wananchi kushirikiana kwa pamoja katika kutii maelekezo na maagizo yanayotolewa na serikali ili kuifanya Ikungi  isonge mbele kimaendeleo.

0 maoni:

Chapisha Maoni