Jumanne, 23 Agosti 2016

Watu sita wamefariki Kutokana na Tetemeko la ardhi nchini ITALIA


Tetemeko la ardhi lenye nguvu ya 6.2 katika vipimo vya Richter limetikisa eneo la Umbria katikati mwa Italia na kufukua watu chini ya vifusi, maafisa wa Italia wamesema.
Tetemeko hilo lilitokea mwendo wa saa tisa na dakika thelathini na sita usiku saa za Italia (01:36 GMT), 76 km (maili 47) kusini mashariki mwa mji wa Perugia, katika kina cha 10km (maili sita) chini ya ardhi, taasisi ya Marekani inayohusika na mitetemeko ya ardhi USGS imesema.
Mitetemeko ilisikika katika miji ya mbali kama vile Roma na Italia. Mjini Roma, baadhi ya majumba yalitikisika kwa sekunde 20, kwa mujibu wa gazeti la La Repubblica.
Watu wanne wameripotiwa kufariki katika eneo la Accumoli, na meya wa mji jirani wa Pescara del Tronto amesema watu wawili wazee walifariki baada ya nyumba yao kuporomoka.
Eneo hilo, ambalo linapakana na mikoa ya Lazio na Marche, ni maarufu sana kwa watalii na kuna wageni wengi waliokuwa eneo hilo kipindi hiki cha shughuli nyingi za kitalii.
Kitovu cha tetemeko hilo kilikuwa katika mji wa Norcia, karibu na Perugia.
Waziri mkuu wa Italia, Matteo Renzi, amesema serikali yake inaendelea kuwasiliana na taasisi za kiraia la ulinzi wa nchi hiyo.
Meya wa mji wa Amatrice Sergio Perozzi ameambia kituo cha redio cha serikali cha RAI kwamba mji huo umeharibiwa vibaya.
"Barabara za kuingia na kutoka mjini hazipitiki. Nusu ya mji imeharibiwa. Watu wamefukiwa chini ya vifusi… kumetokea maporomoko ya ardhi na kuna daraja moja ambalo huenda likaporomoka," amesema.
Shirika la kulinda raia Italia limeeleza tetemeko hilo kuwa "mbaya".
Tetemeko hilo awali lilikisiwa kuwa la ukubwa wa 6.4. Lilifuatwa na mitetemeko mingine mikubwa, gazeti la
La Repubblica limeripoti.
USGS wamesema uharibifu huenda ukawa mkubwa.
Mwaka 2009, tetemeko la ardhi la nguvu ya 6.3 lilitokea eneo la Aquila, na kusikika pia katika mji wa Roma. Watu zaidi ya 300 walifariki.

0 maoni:

Chapisha Maoni