Jumanne, 4 Oktoba 2016

WARIDE: ASISITIZA VIKAO KWA VIONGOZI.

Posted by Esta Malibiche on Oct4.2016 in SIASA

indexNa Is-haka Omar, Zanzibar.
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar  kimewasihi viongozi wa ngazi mbali mbali katika Wilaya ya Kaskazini  “B” kufanya vikao halali vya mara kwa mara ili kuibua na  kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu changamoto zinazowakabili wanachama na  wananchi kwa ujumla.
Nasaha hizo zimetolewa na Katibu wa Kamati Maalum wa NEC, Idara ya Itikadi na uenezi CCM Zanzibar Waride Bakar Jabu wakati akizungumza na wafuasi wa Chama hicho katika  Matawi ya CCM  Boma Kiwengwa na Kinduni  Mahonda katika mwendelezo wa ziara ya kuimarisha chama ndani ya Wilaya hiyo.
Alisema vikao halali vya kikatiba ndani ya Chama hicho ndio jukwaa rasmi la kujadiliana, kushauriana na kufanya maamuzi sahihi ya kulinda na kuimarisha  uhai wa CCM .
Waride alifafanua kwamba  kutokuwepo na vikao kwa baadhi ya ngazi za kiutendaji kunakwamisha utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 20-15/2020 kwa baadhi ya maeneo nchini.
“Sio vizuri mambo yanayohusu Chama chetu yakajadiliwa nje ya vikao halali wakati sehemu rasmi za kufanya hivyo zipo na kama kuna jambo la msingi hakuna anayezuiwa kujenga hoja kupitia vikao, na tukifanya kinyume na hivyo tutatengeneza fitna na migogoro isiyokuwa ya lazima.
Pia kupitia vikao mtaweza kuwa na hoja ya pamoja ya kujibu baadhi ya njama na Propaganda zinazofanywa na wapinzani katika maeneo yenu”,. Alisisitiza Waride na kuongeza kwamba CCM itaendelea kuwa kinara wa siasa za maendeleo na haki endapo kila kiongozi atatekeleza wajibu wake kulingana na majukumu aliyopewa kikatiba.
Alifafanua kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Chama wametekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo nchini lakini imekuwa haijulikani kwa baadhi ya wananchi na viongozi kutokana na kutokuwepo na kutokuwepo na mfumo mzuri wa kupeana taarifa kupitia vikao.
Alisema chama hicho kitahakikisha ahadi mbali mbali zilizoahidiwa katika Uchaguzi Mkuu uliopita zinatekelezwa kabla ya mwaka 2020, ili kila mwananchi aweze kunufaika na fursa zinazotokana na matunda ya Chama hicho.
Katibu huyo aliahidi kuchukua hatua za makusudi kwa kuishawishi serika kuendelea kutafuta wawekezaji wenye nia ya kuwekeza katika sekta za Kilimo, Uvuvi na Utalii ili wananchi hasa wanaoishi vijijini waweze kupata ajira na kuongeza kipato chao.
Kupitia vikao hivyo, Waride aliwakumbusha wananchi umuhimu wa kulinda amani na utulivu wa nchi pamoja na kushirikiana na viongozi wao wa majimbo na serikali katika harakati kukuza uchumi wa Zanzibar.
Akijibu baadhi ya hoja za wanachama wa Chama hicho, Katibu wa Kamati Maalum, Idara ya Organazesheni ya CCM Zanzibar, Haji Mkema aliwataka Wazazi  na Walezi wa CCM ndani ya Wilaya hiyo kuwarithisha Vijana historia na Itikadi halisi za CCM ili wawe waumini wa kweli wa Chama hicho.
Alisisitiza  umuhimu wa wanachama wa chama hicho kutumia fursa zilizowazunguka ndani ya Wilaya hiyo zikiwemo Utalii na kilimo kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira huku wakisubiri  juhudi zinazofanywa na serikali kumaliza tatizo hilo.
Aliwambia na kuwataka vijana wa Chama hicho kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kuwa mfano mwema  wa kuigwa katika jamii kwani wao ndio warithi wa viongozi wanaostaafu utumishi ndani ya chama hicho.
Wakizungumza  wanachama hao,  walikiomba chama kuwachukulia hatua za kinidhamu baadhi ya viongozi wanaofanya kazi za CCM  chini ya kiwango ili kuongeza kasi ya utendaji ndani ya Wilaya hiyo.
Waliwakumbusha Viongozi wa ngazi mbali mbali kutoa taarifa sahihi   kwa wanachama wao juu ya fursa na mambo yanayogusa moja kwa moja uimarishaji wea Chama ili yajulikane kwa wanachama kwa lengo la kuepusha migogo na  makundi yasiyokuwa ya lazima.

0 maoni:

Chapisha Maoni