Jumanne, 16 Agosti 2016

MKUU WA WILAYA KILOLO ASIA ABDALAH AZINDUA WODI YA WAZAZI

Postedy by Esta Malibiche On August 17.2016 in News





MKUU wa wilaya ya Kilolo, Asia Abdalla amezindua wodi ya wazazi iliyojengwa katika Zahanati ya kijiji cha Kiwalamo wilayani humo huku akiahidi kuchangia toka mfukoni mwake harakati za wananchi wa kijiji hicho wanaotaka Zahanati hiyo iwe kituo cha afya.
Wodi hiyo yenye uwezo wa kuchukua vitanda 16 vya kupumzisha wajawazito wakati wakisubiri kujifungua imejengwa kwa msaada wa kampuni ya New Forest, wawekezaji wenye mashamba ya miti yenye ukubwa wa ekari 12,000 wilayani humo.
Akitoa taarifa ya ujenzi wa wodi hiyo, Afisa Mahusiano na Maendeleo ya Jamii wa kampuni hiyo, Robert Nyachia alisema imejengwa kwa Sh Milioni 49.7 ambazo kati yake Sh Milioni 44.7 ni mchango wa kampuni yao na Sh Milioni 5 ni mchango wa wananchi.
Nyachia alisema New Forest imechangia ujenzi huo huku ikitambua umuhimu wa upatikanji wa huduma za afya kwa wote kama inavyosisitizwa katika Mipango ya Maendeleo Endelevu ya Dunia (SDGs).

Katika kuhakikisha inaanza kutoa huduma zake, Kaimu Mganga wa Wilaya ya Kilolo, Dk Ibrahim Kisaka alisema halmashauri ya wilaya hiyo imetumia Sh Milioni 4 kuwezesha wodi hiyo kuwa na baadhi ya vifaa tiba na dawa muhimu.
Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho, Ebineda William alisema; “kujengwa kwa wodi hiyo ni mkombizi kwao kwani wazazi wengi tulikuwa tunalazimika kutumia gharama kubwa kufuata huduma za uzazi zinazokosekana katika zahanati hii katika kituo cha afya Bomalang’ombe au mjini Iringa.”
Akizundua wodi hiyo, DC Abdalla alisema itasaidia kupunguza au kumaliza tatizo la baadhi ya wajawazito kujifungulia majumbani au mbali na kijiji hicho kwasababu ya kukosekana kwa huduma hiyo.
“Nawaagiza viongozi wa serikali katika kijiji hiki na vijiji jirani kuwahamasisha wajawazito kuja hapa kupata huduma ya kliniki na zingine zitakazotolewa katika wodi hii, tukilenga kuzuia vifo vya mama na mtoto kwasababu ya ukosefu wa huduma,” alisema.
Mkuu huyo wa wilaya aliyepokelewa na wananchi ambao baadhi yao walikuwa na mabango yanayotaka Zahanati hiyo iboreshwe ili iwe kituo cha afya alisema; “nimesikia ombi lenu la kuwa na huduma bora kabisa za afya, inawezekana mkawa na kituo cha afya lakini ni lazima mkidhi vigezo vyake vyote.”
Alisema yeye binafsi yupo tayari kutoa sehemu ya mshahara wake kuchangia harakati hizo endapo wananchi wa kijiji hicho watakuwa tayari kuchangia ujenzi wa majengo mengine muhimu yatakayoifanya Zahanati hiyo iwe na sifa ya kuwa kituo cha afya.
Wakimjibu mkuu wa wilaya huyo, wananchi waliojitokeza kwa wingi kushuhudia uzinduzi wa wodi hiyo walisema wapo tayari kuchangia ujenzi wa majengo ya ziada na mahitaji mengine yatakayowawezesha kuifanya zahanati yao iwe na hadhi ya kituo cha afya.

Kaimu Mkurugenzi wa wilaya hiyo, Hellen Chissanga alitaja vigezo mbalimbali muhimu kwa ajili ya uanzishaji wa kituo cha afya ikiwa ni pamoja na kuwa na chumba cha upasuaji.

0 maoni:

Chapisha Maoni