Jumatano, 10 Agosti 2016

WASIMAMIZI WA MIRADI YA TEHAMA SERIKALINI WAPEWA MAFUNZO

Postedy by Esta Malibiche on August 10.2016

KATU1
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Arnold Mathoyo akieleza utaratibu wa mafunzo ya TEHAMA kwa washiriki wanaosimamia miradi ya TEHAMA chini ya Mradi wa Miundombinu ya Mawasiliano (RCIP) Tanzania katika ukumbi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Dodoma.(James Katubuka Mwanamyoto)
KATU2
Washiriki wa mafunzo kuhusu TEHAMA wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Susan Mlawi (hayupo pichani).
KATU3
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Susan Mlawi i akifungua mafunzo kwa wataalam wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wanaosimamia miradi chini ya Mradi wa Miundombinu ya Mawasiliano (RCIP) Tanzania katika ukumbi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Dodoma.
KATU4
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Susan Mlawi akisisitiza jambo wakati akifungua mafunzo kwa wataalam wa TEHAMA wanaosimamia miradi chini ya Mradi wa Miundombinu ya Mawasiliano (RCIP) Tanzania katika ukumbi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Dodoma.
………………………………………………………………………………………
Usimamizi na utekelezaji wa Serikali Mtandao unahitaji Rasilimaliwatu yenye weledi mkubwa wa kusimamia maeneo ya msingi.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Susan Mlawi alisema hayo mkoani Dodoma wakati akifungua mafunzo kwa wasimamizi wa miradi mbalimbali ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) inayotekelezwa chini ya Mradi wa Miundombinu ya Mawasiliano (RCIP) Tanzania.
“ Rasilimaliwatu katika eneo hili inahitaji kupewa mafunzo na kuendelezwa katika nyanja muhimu za usimamizi wa TEHAMA na pia kuwa na uwezo na uelewa wa mifumo na taratibu za utendaji kazi katika Taasisi za Umma” Bi. Mlawi alisema.
Bi. Mlawi alifafanua kuwa, mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa lengo la Serikali la kuwajengea uwezo wataalam wake ili kuboresha utekelezaji wa miradi ya Serikali Mtandao yenye lengo la kuziwezesha Taasisi za Umma kutoa huduma bora kwa Wananchi.
Aliongeza kuwa, mafunzo hayo yamelenga kuongeza uwezo kwa wataalam wa Serikali hususani katika Ununuzi  na usimamizi wa utekelezaji wa mifumo na mitandao mbalimbali ya TEHAMA inayowekwa katika Taasisi za Serikali ili kuboresha utendaji kazi na utoaji wa huduma kwa Umma.
 Bi. Mlawi aliainisha kuwa uteuzi wa washiriki wa mafunzo hayo umezingatia ushiriki katika utekelezaji wa miradi ya RCIP na matokeo ya utafiti wa mahitaji ya mafunzo kwa maafisa TEHAMA wa Taasisi za Serikali, uliofanywa na Wakala ya Serikali Mtandao (eGA) mwezi  Septemba, 2015.
Alisisitiza kuwa, kila mshiriki atajengewa uwezo wa kiufundi kulingana na mahitaji halisi katika eneo au maeneo ya kusimamia na kutengeneza mifumo ya TEHAMA.
Naibu Katibu Mkuu huyo Bi. Mlawi, alielekeza washiriki wa mafunzo hayo wahakikishe ujuzi watakaoupata unawafikia wale ambao hawakubahatika kuchaguliwa kwa sababu idadi ya washiriki walioteuliwa kuhudhuria mafunzo ni ndogo ikilinganishwa ya idadi kubwa ya Maafisa TEHAMA waliopo katika Taasisi za Serikali  ili kwa pamoja  washirikiane kubuni mifumo ya TEHAMA yenye kuboresha  utendaji kazi na utoaji  huduma kwa umma. 
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ina jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa miradi ya RCIP eneo la Mifumo ya Serikali Mtandao “e-Government Applications” ambapo mifumo mbalimbali ya TEHAMA (ya Kimkakati na ya Kisekta) inaendelea kuwekwa na kutekelezwa katika Taasisi walizotoka washiriki wa mafunzo.
Mifumo hiyo ni  Mfumo wa Wakala ya Usajili, Vizazi na Vifo (Birth and Death Registration System) kupitia Wakala ya RITA; Mfumo wa Taarifa za Biashara (National Business Portal) kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara, Mfumo wa Taarifa za Kitabibu (Telemedicine system) kupitia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Mfumo wa Taarifa za Ununuzi (e-Procurement system) kupitia Mamlaka ya Uthibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA)  na Bohari ya Dawa (MSD), Mradi wa “electronic Records” kupitia Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa na; Mradi wa “electronic Office” kupitia Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma, na Wakala ya Serikali Mtandao (eGA).
Mafunzo hayo yatatolewa kwa Maafisa,  Wasimamizi wa miradi 62; Wakuu wa Vitengo vya TEHAMA 15  na Maafisa Ugavi  50 kutoka kwenye Taasisi mbalimbali za Serikali na yatafanyika kwa awamu 5 katika ukumbi wa  Mikutano wa Idara ya  Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa Dodoma.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Ofisi ya Rais-UTUMISHI

0 maoni:

Chapisha Maoni