Jumatatu, 15 Agosti 2016

Rubani Precision Air akikubali kiwanja cha ndege cha Dodoma

AT1
Rubani Kevin Chibole wa Shirika la ndege la Precision baada ya kutua kwenye kiwanja cha ndege cha Dodoma hivi karibuni.
AT2
Ndege ya shirika la ndege ya Precision baada ya kutua kwenye kiwanja cha ndege cha Dodoma baada ya kurefushwa kwa barabara ya kuruka na kutua kutoka kilometa 2 hadi kufikia kilometa 2.5. 
………………………………………………………………………..
RUBANI Kevin Chibole wa shirika la ndege la Precision, amesema atawashawishi waajiri wake, kuanza safari za kutoka Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) kilichopo jijini Dar es Salaam na kwenda kiwanja cha ndege cha Dodoma, kwani sasa barabara yake ya kutua na kuruka kwa ndege imerefushwa zaidi.
Chibole, aliyerusha ndege ATR 72 5H PWA, amesema awali walishindwa kufanya safari kwenye kiwanja cha ndege cha Dodoma, kutokana na barabara yake ya kutua na kuruka ndege kuwa fupi kwa urefu wa kilometa  2, lakini sasa imerefushwa hadi kufika kilometa 2.5, itakayoruhusu ndege kubwa kutua na kuruka bila tatizo.
“Hii runway (barabara ya kutua na kuruka ndege) ni nzuri haina mabondebonde, hivyo sasa umefika wakati muafaka kuwaeleza wamiliki wa ndege hii, tuanze safari ya hapa Dodoma kwa kutokea JNIA,” alisema Chibole.
Naye Waziri wa Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utawala Bora na Utumishi wa Umma wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe, Harun Ally Suleiman aliyekuwa miongoni mwa abiria 37 waliokuwa wamepanda ndege hiyo iliyotoka kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Amani Abeid Karume (AAKIA) Zanzibar na kutua JNIA na baadaye kuanza safari ya Dodoma, alisema hakuwahi kwenda Dodoma kwa ndege kubwa, na safari hiyo imekuwa ya kwanza kwake.
“Tunaishukuru Serikali ya Rais Magufuli, kwani tunaona kunaujenzi unaoendelea hapa na hata tumeambiwa kuwa hii barabara tuliyotua na ndege ya Precision imeongezwa urefu na ndio maana ndege hii ikaweza kutua, tunashukuru sana kwa hili,” alisema Mhe. Harun. 
Amesema miundombinu ya usafiri ikiboreshwa itasaidia eneo husika kukuza uchumi wake, ambapo sasa Dodoma itakuwa juu kiuchumi kwa kuwa tayari wafanyabiashara watatumia zaidi usafiri wa ndege kwa kuwa ni wa haraka na uhakika.
Pia abiria mwingine aliyesafiri kwa ndege hiyo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Riziki Pembe Juma alisema kuwa awali wajumbe wa mkutano mkuu wa Chama tawala kutoka Zanzibar, walikuwa wakitumia zaidi usafiri kwa barabara, kutokana Dar es Salaam hadi Dodoma kutokana na kutokuwa na ndege kubwa ya kutosheleza wajumbe wote kwa pamoja, ila kurefushwa kwa barabara ya kutua na kuruka imekuwa faraja na kufanya safari kuwa fupi na haraka.
“Naona namna gani Serikali ya Awamu ya Tano, inavyotekeleza kwa kasi ahadi zake, na hii ni mojawapo ya upanuzi wa kiwanja, ambapo kitaleta tija kwa wakazi wa hapa na nchi nzima kwa ujumla,” alisema Mhe. Riziki.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mhandisi George Sambali alisema kutua vizuri kwa ndege ya shirika la ndege la Precision ATR 72 5H PWA kutachochea ongezeko la ndege kubwa zaidi zenye uwezo wa kubeba abiria kuanzia 50 hadi 90 kutua kwenye kiwanja cha ndege cha Dodoma.
“Tuliambiwa na Mh. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa wakati akiweka jiwe la msingi la ukarabati na upanuzi wa kiwanja hiki cha Dodoma, kuwa hapa patakuwa ni kitovu cha shughuli mbalimbali hivyo zitaanza kuja ndege kubwa zikiwemo za ATCL zinazotarajiwa kuwasili nchini Septemba 2016, hivyo ni matumaini yangu kuwa hata bei ya safari itashuka maana zitakuwa nyingi,” alisema Mhandisi Sambali.
Wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la mradi wa ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Dodoma, uliofanyika hivi karibuni Mh. Waziri Mkuu, Kassim M. Majaliwa alisema kutokana na kurefushwa kwa barabara hiyo, sasa kiwanja hiki kitakuwa na uwezo wa kupokea ndege kubwa za ATCL, Precision na Fastjet, na gharama itapungua.
Kazi ya ukarabati na upanuzi huo inayosimamiwa na timu ya Wahandisi wazawa wanaoogozwa na Mhandisi Mbila Mdemu kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), huku mkandarasi akiwa ni Kampuni ya China Henan International Cooperation (CHICO) Group Co. Ltd kutoka Jamhuri ya watu wa China. Tayari ujenzi umekamilika kwa asilimia 65, ambapo hivi karibuni Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe, Prof. Makame Mbarawa, aliyetembelea kuona maendeleo ya kazi hiyo iliyoanza siku 45 zilizopita.
“Mradi huu umetupa mfano kama tukijipanga vizuri hata kwenye miradi mingine tunaweza kutekeleza kwa haraka na ubora unaotakiwa, kwa upande wetu kama Serikali tutahakikisha kiwanja hiki kinakamilika haraka ili kuruhusu ndege kubwa kuanza kutua”, amesisitiza Waziri Mbarawa.
Aidha ameongeza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa uwanja huo utakuwa chachu kwa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL)  kuwaunganisha watanzania  kwa kutoa huduma za usafiri anga katika maeneo mbalimbali nchini na hivyo kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi wa nchi.
Kwa upande wake Meneja Mradi wa upanuzi huo Mdemu amesema mpaka sasa mita 2450 zimekamilika kwa kuweka tabaka la kwanza lami katika eneo la kuruka na kutua ndege.
“Kasi ya ujenzi wa kiwanja hiki inaendelea vizuri kwa kushirikiana na mkandarasi wa kampuni ya CHICO na kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa wakati kwa kuzingatia viwango na ubora unaotakiwa”, amesema Mhandisi Mdemu.
Upanuzi wa uwanja wa ndege wa Dodoma  unahusisha njia ya kuruka na kutua kwa ndege yenye urefu wa Km 2.5, barabara za viungio na maegesho ya ndege.

0 maoni:

Chapisha Maoni