Jumatano, 6 Julai 2016

MBUNGE WA VM AYSHAROSE ATOA MADAWATI 100

 Baadhi ya Madawati yaliyokabidhiwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida.
Mkuu wa mkoa wa Singida  Mhandisi Mathew Mtigumwe akizungumza wakati wa kukabidhiwa msaada huo.

 MBUNGE wa Viti Maalumu Mkoa wa Singida, Aysharose Mattembe, ametoa amekabidhi msaada wa madawati 100 kwa ajili ya kusaidia kukabiliana na tatizo hilo kwenye shule za Halmashauri ya Wilaya ya Singida Vijijini.

Msaada huo wa madawati kwa Singida Vijijini ni sehemu ya jitihada za mbunge huyo kusaidia jamii, ambapo anatarajia kuzifikia wilaya zote za mkoa huo ili kuwawezesha wanafunzi kusoma kwa utulivu.

Akizungumza juzi katika hafla fupi ya makabidhiano hayo kwenye Viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Aysharose alisema msaada huo ni utekelezaji wa agizo la Rais Dk. John Magufuli la kutaka Watanzania kusadia kukabiliana na uhaba wa madawati katika shule za msingi na sekondari nchini.

Alisema wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu Dk. Magufuli aliahidi kwamba serikali yake itahakikisha elimu kuanzia msingi hadi kidato cha nne itakuwa bure, jambo ambalo limetekelezwa kwa mafanikio makubwa, lakini limekuja na changamoto zake ikiwemo uhaba wa madawati kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi waliandikishwa shuleni.

“Elimu yetu sasa ni bure ili kuwawezesha watoto wote kusoma, lakini sera hii imekuja na changamoto zake ambazo jamii ni lazima tushiriki kuzipatia ufumbuzi. Kuna uhaba wa madawati, nyumba za walimu na vitendea kazi vingine. Nimeanza na madawati kwa Singida Vijijini na nitaendelea kujibana na kutumia kidogo ninachopata na nitazifikia wilaya zote za mkoa wangu,” alisema Aysharose.

Hata hivyo, alisema Singida inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo miundombinu, afya na uwezeshaji wanawake na vijana kiuchumi na kwamba, amejipanga kupambana kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi.

“Nitajitahidi kutekeleza ahadi zangu kwenye sekta mbalimbali ikiwemo afya, maji na miundombinu kadri Mungu atakavyonijali afya njema na uwezo. Niombe tu tutunze madawati haya ili kusaidia watoto wetu na yafikishwe kwenye shule ambazo zinaonekana kuwa na tatizo kubwa.

Naye mgeni rasmi kwenye hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhandisi Mathew Mtigumwe, alimpongeza Aysharose kwa kutekeleza Ilani ya CCM kwa vitendo na kuwa ni mbunge anayewajibika kikamilifu kwa jamii yake.

“Nimpongeze Mheshimiwa Aysharose kwa kazi kubwa anayoifanya kupigania maendeleo kwenye mkoa wetu. Ni matarajio yetu madawati haya yatasaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi na kuchochea ongezeko la ufaulu.
“Aysharose ni mpambanaji mzuri na serikali ya mkoa tunakupongeza sana kwa utendaji kazi wako wa vitendo,” alisema Mhandisi Mtigumwe.

Alisema kwa sasa uhaba wa madawati mkoani Singida umepungua kwa kiasi kikubwa, ambapo wananchi wamehamasisha na kujitokeza kusaidia. 

“Kwa sasa tumebakiwa na uhaba mdogo sana wa madawati. Mikakati iliyopo ni kwamba hadi Julai 15, mwaka huu, tutakuwa tumemaliza kabisa tatizo hili na tunatarajia kuwa na ziada ya madawati kwa shule zetu za msingi na sekondari,” alisema.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Singida Vijijini, Elia Elia Digha, alimpongeza mbunge Aysharose kwa msaada huo na kumhakikishia kuwa madawati hayo yatatunzwa vizuri ili yaweze kutumika kwa muda mrefu.

“Mheshimiwa Aysharose tunakupongeza na kukushuruku sana kwa msaada huu na tunakuhakikishia madawati haya yatatunzwa vizuri. Utaendelea kukumbukwa daima kwa msada huu ambao una manufaa makubwa kwa watoto wetu. Mwenyezi Mungu akulinde na akuongoze kwenye utekelezaji wa majukumu yako,” alisema Digha, ambaye ni Diwani wa Kata ya Msange.

0 maoni:

Chapisha Maoni