……………………………………………………………………………………………..
Na Benny Mwaipaja,MoFP
SERIKALI za Tanzania na Korea
Kusini, zimetiliana saini Hati ya Makubaliano (Aide Memoire) kwa ajili
ya Ushirikiano wa utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya maendeleo ukiwemo
wa Maji, Nishati, Kilimo, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA na
Viwanda itakayogharimu Dola za Marekani Milioni 300, sawa na
TSh.Bilioni 650, katika kipindi cha miaka mitano ijayo kuanzia mwaka
2016 hadi 2020.
Fedha hizo ni sawa na ongezeko la
Dola Milioni 100 ikilinganishwa na kiasi cha Dola Milioni 200 ambazo
nchi hiyo ya Korea iliipatia Tanzania kama mkopo wenye masharti nafuu
katika kipindi cha miaka miwili iliyopita (2014 hadi 2016).
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya
Fedha na Mipango, Bi. Amina Shaaban, ametia saini makubaliano hayo kwa
niaba ya Serikali ya Tanzania, huku upande wa Korea Kusini ukiwakilishwa
na Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Fedha ya Korea Bw. Weon-Kyoung Jo.
Kusainiwa kwa makubaliano hayo ni
mwanzo wa matayarisho ya kuandaa Mpango kazi wa namna ya kutekeleza
miradi hiyo ili iende sambamba na Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo
wa miaka 5 uliozinduliwa hivi karibuni mjini Dodoma na Waziri Mkuu, Mhe.
Kassim Majaliwa na Mkakati Mbadala wa Kupunguza Umaskini Zanzibar
(MKUZA Successor Strategy).
Akizungumza mara baada ya
kusainiwa kwa makubaliano hayo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na
Mipango, Bi. Amina Shaaban, amesema kuwa miradi hiyo ya maendeleo
iliyochaguliwa kutekelezwa katika sekta zilizotajwa zitachochea ukuaji
wa uchumi wa Taifa na kupunguza umasikini kwa wananchi.
Bi. Amina Shaaban alisema kwamba
Hati hiyo ya Makubaliano ya ushirikiano kati ya Tanzania na Korea
Kusini, yamejikita zaidi katika uboreshaji wa mifumo ya Tehama,
kuimarisha sekta ya kilimo pamoja na kuboresha miundombinu inayosaidia
ukuaji wa viwanda hususan ya nishati ya umeme katika kipindi cha kuanzia
mwaka wa fedha 2016/17 hadi 2020/21.
“Ushirikiano wa Tanzania na Korea
Kusini umeanza tangu mwaka 2000, kwa kuhusisha taasisi zake mbili
ambazo ni Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA) ambalo
limeipatia Tanzania kiasi cha zaidi ya dola za Marekani 30.9 na Benki ya
Exim-Korea ambayo imetoa Dola za Marekani zaidi ya Milioni 455 sawa na
zaidi ya Tsh 900 bilioni kwa ajili ya miradi mbalimbali ya kiuchumi na
kijamii katika kipindi cha miaka 10 iliyopita” alisema Bi. Amina Shaaban
Ametoa wito kwa nchi hiyo
kuwekeza hapa nchini kutokana na fursa mbalimbali zilizopo za kiuchumi
zikiwemo mazingira mazuri ya uwekezaji, rasilimali za kutosha ikiwemo
gesi asilia, madini, sekta ya utalii, hali nzuri ya hewa pamoja na amani
na utulivu.
Akizungumza katika tukio hilo
Weon-Kyoung Jo, amesema kuwa Tanzania inaongoza katika bara la Afrika
kupata misaada na mikopo nafuu kutoka Korea Kusini baada ya nchi hiyo
kuridhishwa na mipango mizuri ya maendeleo iliyowekwa na Serikali ya
Tanzania.
Amesema kwamba vipaumbele
vilivyowekwa na Serikali ya Awamu ya Tano zikiwemo Sekta za Viwanda,
Kilimo na TEHAMA vinaungwa mkono na nchi yake na kwamba wako tayari
kusaidia kwa njia ya kutoa ruzuku na mikopo yenye masharti nafuu.
Kwa upande wake, Naibu Katibu
Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kikanda, Afrika Mashariki na
Kimataifa, Balozi Ramadhan Mwinyi, amesema kuwa serikali ya Tanzania
inatarajia kufungua ubalozi wake nchini Korea Kusini ili kuimarisha
ushirikiano uliopo kati ya nchi hizo mbili.
0 maoni:
Chapisha Maoni